Monday, February 9, 2015

UNAKUWA MASKINI KADILI UNAVYOCHELEWA KUPATA FEDHA INAYOFUATA BAADA YA KUPATA LEO



Ukifuatilia na kutafakari suala zima la mapato na matumizi ya pesa kwa watu walio wengi, utagundua kuwa kuna tatizo kubwa la msingi. Fikiria mkulima wa Tanzania ambaye amebahatika kuishi maeneo yenye misimu miwili ya mvua wanapata Mazao mara mbili kwa mwaka, hii ikiwa na maana kwamba, anapata fedha mara mbili kwa mwaka, maana yake mtu huyu akipata pesa leo, pesa nyingine itapatikana baada ya miezi sita. Lakini kwa mkulima anayeishi maeneo yenye msimu mmoja wa mvua, wanapata mavuno mara moja kwa mwaka mzima, hii ikimaanisha kuwa huyu mtu anapata pesa mara moja kwa mwaka. Wafanyakazi na hasa wa serikali na makampuni binafsi wana pata fedha kila mwezi. Wafanyabiashara wadogo na wa kati wanapata pesa kwa wiki na wengine kila siku. Wafanyabiashara wakubwa na matajiri wengine wanapata pesa kwa saa, dakika na wengine kama makampuni ya simu wanapata hadi kwa sekunde.

Uzoefu umeonyesha kuwa unapochukua muda mrefu kuingiza pesa nyingine ndivyo unakuwa maskini wa kutupwa na maisha yanakuwa magumu kweli kweli. Sababu kubwa ya umaskini huo ni kutokana na ukweli kwamba mahitaji au matumizi ya mtu yeyote huwa ni kila siku na wakati huo huo mapato ni kwa mwaka au kila baada ya miezi sita kwa Wakulima walio wengi. Kutokana na hali hii tunaona kuwa hakuna ulinganifu ulio sawa kati ya kupata na kutumia pesa. Kupishana kwa mapato na matumizi ndiko kunakofanya watu wengi na hasa Wakulima kuishi Katika madeni makubwa ambapo inapofika msimu wa mavuno Wakulima hawa tayari wanakuwa wanadaiwa, kiasi kwamba inapotokea msimu haukwenda vizuri wengine ulazimika kuuza hata vipande vya ardhi waliyokuwa nayo ili kulipa madeni, wengine huwa hawasubili kuvuna ndipo wauze badala yake wanauza Mazao yao ya yakiwa bado kukomaa shambani.

Katika wilaya za Karagwe, Bukoba na Muleba ambako zao la kahawa linalimwa kwa wingi Wakulima wengi uchukua fedha kama mkopo kutoka kwa wafanyabiashara kabla ya kahawa kukomaa wenyeji wanaita “Butura”. Biashara ya “Butura” ni maarufu sana mkoani Kagera. Watu upewa pesa kabla ya Mazao kukomaa huku wakikubaliana kulipana Mazao pindi yakikomaa. Katika Wilaya ya Ngara wao huuza mahindi yakiwa hata bado kubeba, maeneo ya usukumani suala hili liko sana kwenye zao la mpunga japo wengi uwa wanakopa pesa kutoka kwa wafanyabiashara ili kupata pesa ya palizi na kuhemea ndege“kumoja” n.k.

Kwasababu wanachukua muda mrefu kupata pesa, ndiyo maana wakishapata pesa wanachangamka sana kuzidi kipimo na hii ni kutokana na sababu kuwa mara nyingi wakati wa msimu, pesa uja kwa mkupuo, hali ambayo huwafanya kuzitumia ovyoovyo na wengine ujaribu na kuongeza mke wa pili, kunywa pombe kupindukia, harusi na sherehe nyingi. Kutokana na matumizi ambayo uambatana na mihemuko ya kila aina, watu uweza kuishiwa pesa walizokuwa nazo mara tu baada ya takribani mwezi mmoja hadi miwili.

Baada ya watu kuishiwa pesa zilizotokana na mavuno, watu wengi hurudia hali yao ya kutokuwa na pesa na hapa ndipo, utaanza kusikia lugha za “hakuna mzunguko wa pesa” Eti kila mmoja anaanza kusema pesa hakuna siku siku hizi; Kumbe kiuhalisia siyo kwamba hakuna pesa, isipokuwa ni kwamba hakuna cha kuuza wakati huo. Pesa huwa inafuata vitu vilipo pamoja na huduma zilipo. Hali hii ujenga hofu sana miongoni mwa wanajamii hasa kutoka Katika kaya masikni na pia kukata tamaa. 

Kutokana na hofu na imani kwamba kijjini hakuna pesa, wengi wao na hasa vijana uchukua uamzi wa kukimbilia mijini wanakoamini kuna mzunguko wa pesa wasijue kuwa hata huko wanakoamini kuwa na mzunguko mzuri wa pesa bado utalazimika kuwa na vitu au huduma ndipo uzipate, bila kuwa na vitu/huduma – wewe hata kama uko mjini unakoamini kuwa kuna mzunguko wa pesa, bado pesa utaziona tu kwa wengine na si kwako!!!!.

Kwahiyo kama wewe ni mmoja wa wadau wa maendeleo, njia pekee ya kuwakomboa Wakulima ni pamoja na kutafuta njia ya kufupisha muda wa kupata fedha nyingine angalau ukiweza kushuka kutoka miezi sita mpaka mwezi mmoja. Hikiwa hivi ndivyo, basi itakuwa ni hatua moja muhimu sana Katika kupambana na umaskini hasa Wakulima.

Mpendwa msomaji endelea kuitumia vizuri MAARIFASHOP, ili kujifunza mambo mbalimbali yatakayokuwezesha kufanikiwa. Kupata makala mpya kila zinapochapishwa, bonyeza sasahivi neno- hivi; TUMA MAKALA MAARIFASHOP kisha sajiri barua pepe yako na kama unapenda kupata mafunzo ya kila siku na makala mpya kwa njia ya whatsap bonyeza neno MAFUNZO

KARIBU TUCHUKUE HATUA PAMOJA!!

No comments: