Kiongozi


Unafahamu Makosa ni Mfuko Ulioficha Vitu Vizuri?




Kwenye mchakato wa biashara, ujasiriamali na maisha kwa ujumla, kuna makosa mengi yanayoendelea kufanyika. Wakati mwingine utulazimu kulipa gharama kubwa, ili kurekebisha makosa yaliyofanyika. Kwahiyo, tuseme kwamba makosa ni gharama, ndiyo maana wengi ujitahidi sana kukwepa kufanya makosa—Japo bado wanafanya makosa!! Lakini,
uzoefu umeonyesha kuwa, pamoja na kulipa gharama zitokanazo na makosa fulani fulani bado makosa hayo hayo ni fursa nzuri sana ya kujifunza na kuweza kuwa bora zaidi. Hapa chini kuna mfano halisi wa jinsi nilivyoweza kujifunza kitu kikubwa baada ya kufanya makosa:

Siku ya Jumapili ya tarehe 12/11/2017, nilisafiri kutoka Nyakanazi (Biharamulo) kwenda Kasulu (Kigoma). Mara likatokea basi kutoka Kahama, nikaamua kwenda kuuliza kama inawezekana kusafiri na basi hilo. Kondakta aliponiona kama mtu mwenye nia ya kusafiri, akaniwahi kwa kuniuliza ninakokwenda. Kusikia hivyo bila hata ya kutafakari nikamwambia nakwenda Kasulu, naye akasema nauli hadi Kasulu ni shilingi 15,000/-. 
Baada ya kulipa nauli niliingia kwenye gari na safari ikaanza mara moja. Kwa mshangao mkubwa, tulipofika stendi kuu ya mabasi mjini Kibondo, tukaambiwa mwisho wa gari ni hapo stendi na wakasema abiria wote tuliolipia nauli ya moja kwa moja hadi Kasulu, tuingie kwenye gari (TOYOTA ICE), ambalo lilikuwa limepaki pembeni tayari kwenda Kasulu. Hapa ndo kusema kuwa “tulifaulishwa”. Baada ya kupanda ICE hiyo, ndipo nikagundua kuwa wale tuliofaurishwa, tulikuwa ni wachache (watu wanne tu). Changamoto ikawa ni kwamba, lazima tusubili abiria wengine waje kujaza gari ndipo liweze kuanza safari ya kuelekea Kasulu. Kwa jinsi ilivyokuwa siku ya jumapili, niliona kwa haraka haraka niliona hiyo ICE itachelewa sana kuondoka (labda saa kumi jioni badala ya kuondoka saa sita na nusu mchana). Baada ya kukaa stendi kwa muda wa saa nzima bila kuona abiria anayekuja kupanda ICE hiyo, ndipo nilianza kulaumu na kulaani, nikajiuliza maswali mengi yasiyokuwa na majibu; “kwanini hawa vijana wamenifanyia yote haya”? Hawajanitendea haki”, “wamenidanganya” …... nikawa na kila aina ya malalamiko yote unayoyajua.
Baada ya muda akiri yangu ilifunguka nikagundua nimefanya MAKOSA makubwa wakati wa kulipa nauli. Nilitakiwa kulipa nauli hadi Kibondo, nauli inayobaki ningepanda gari ambalo ningeona linafaa kupanda. Kimsingi, mimi ndiye nilikuwa mjinga, kwasababu sikujua taratibu na kanuni zisizo rasimi kwenye sekta ya usafirishaji wa abiria. Nilitakiwa kuuliza mwisho wa basi ni wapi—sikufanya hivyo, badala yake, niliishia kujibu kile nilichoulizwa na kondakta. (kondakta: unasafiri kwenda wapi? Mimi: Kasulu; kondakta: nauli ni 15,000/-; lipa nauli tiketi hii hapa; Mimi: Nikalipa….).
Baada ya kukiri makosa yangu kwenye usafiri niliamua kuwajibika kwa kulipa tena nauli ya shilingi 8,000/- na nikapanda BASI JINGINE lililokuwa likitokea Mwanza ambalo lilisimama stendi (Kibondo) kushusha abiria. Safari hii sikufanya kosa nilikuwa wa kwanza kumuuliza kondakta kama basi lake linafika Kasulu.

Ukifuatilia kisa hiki kizima utaona ni kama vile nililipa shilingi 8,000/- zaidi. Lakini, ukweli ni kwamba pesa hiyo haikulipwa kama nauli bali kama gharama au hada (karo) ya mwanafunzi ambaye alitakiwa kulipia masomo na kupata majibu ya kile ambacho nilikuwa sijui kwenye masuala yote yanayohusu usafiri hasa wa magari ya kuungaunga (kupokezana vijiti).

Baada ya akiri yangu kuichukulia shilingi 8,000/- kama “hada/karo” ya kufuta ujinga, hali ile ya kulalamikia upotevu wa pesa haikuwepo tena. Niliona ilikuwa ni haki hizo pesa zaidi nizilipe, kwasababu, kuanzia siku hiyo nilikuwa tayari nimejifunza jinsi ya kuwa makini wakati wa safari hasa unapotumia magari ya kuungaunga.

Jifunze Kubadili Makosa Kuwa Masomo
Ukiyachukulia makosa kama masomo, uwezo wako wa kutatua au kurekebisha makosa yako unaongezeka. Mfano mzuri ni kama nilivyoeleza hapo juu, endapo siku hiyo nisingeamua kulichukulia KOSA langu kama somo, pengine ningechelewa sana kwenda nilikokuwa naenda. Kwasababu ningeona ni kupoteza pesa kwa kulipa nauli mara mbili.

Sisi kama viongozi wa maisha yetu, ni muhimu sana kuyachukulia makosa kama fursa ya kujifunza kitu kipya juu ya hicho unachofanya, iwe ni kwenye maisha au biashara. Katika kitabu cha “Before You Quit Your Job” (bofya KITABU kupata nakala)—Bwana Robert Kiyosaki anasema; makosa ni kama alama za barabarani zinazoamrisha kusimama. Kwamba makosa ni kama yanakwambia “wewe, sasa ni muda wa kusimama…. tulia kidogo…. kuna kitu hujui …. Ni wakati wa kuacha na kufikiri kwanza. Bwana “Kiyosaki” pia anaendelea kusema kwamba “makosa ni ishara inayokuonyesha kwamba sasa ni muda wa kujifunza kitu kipya ambacho ulikuwa hukijui hapo mwanzo”

Kwahiyo, kila wakati unapofanya makosa, simama, chukua hatua ya kujifunza kitu kipya. Kama kuna kitu hakiendi vizuri kwa jinsi ulivyotegemea au kimekwenda kinyume na matarajio yako, jipe muda wa kufikiri kwa kina. Ukishagundua somo lililokuwa limejificha ndani ya mfuko wa makosa, lazima utakuwa mwenye shukrani kwa makosa hayo. 
 Kama ikitokea ukaona kwamba umeudhika, umekasirika, umehaibika, umelaumu mtu mwingine kwa makosa yaliyofanyika na wewe pia kujifanya kwamba hujafanya makosa yoyote, hapo ujue kuwa hujafikiri sawa sawa. Uwezo wako wa kufikiri bado haujapanuka vyakutosha. Hujajifunza somo lolote kutokana na makosa. Kwahiyo, endelea kufikiri zaidi, kwasababu kadiri utakavyoendelea kufikiri ndivyo unavyozidi kufungua mfuko wa makosa ambao ndani yake kuna (masomo, ukweli, fursa n.k) juu ya kile kinachokutatiza.
 
Waajiriwa na Wajasiriamali Wana Falsafa Gani Juu ya Makosa?
Waajiriwa na wajasiriamali ni watu wanaoishi dunia mbili tofauti na falsafa yao juu ya neno “makosa” ni tofauti sana. Kwa waajiriwa kufanya makosa ina maana kwamba kuna kitu hujui kabisa na wewe ni mjinga. Ndiyo maana mwajiriwa yeyote akifanya makosa, mara nyingi anajifanya hajafanya makosa yoyote; anakataa na anasema makosa yamefanywa na watu wengine siyo yeye. Mwajiriwa atafanya kulaumu wengine juu ya makosa yake—Jambo hili lipo sana kwenye maofisi mengi ya umma na ya watu binafsi.




Ni waajiriwa wachache sana wanaochukulia makosa kama fursa ya kujifunza na kuongeza uwezo wao wa kufikiri. Kila mara waajiriwa tunakuwa makini hadi kupitiliza, huku tukijitahidi kukwepa kufanya makosa, kwasababu tunaamini makosa nikitu kibaya sana. 

Kwa maneno mengine ni kwamba watu wengi wanaoishi kwa kukwepa kufanya makosa mara nyingi ni watu wa kulaumu na kulalamikia wengine. Watu wa namna hii ni wagumu sana kukubali kwamba wamefanya makosa, matokeo yake huwa ni vigumu sana kwao kupata muhafaka wa makosa yaliyotendeka jambo ambalo husababisha makosa yale yale kujirudia mara kwa mara.

Wajasiriamali wao wanaamini makosa ni kitu kinatokea nje ya ufahamu wako ulionao kwa wakati huo. Pia, wanaamini makosa ni kitu ambacho kinaweza kumtokea mtu yeyote bila kujali kisomo, umri na uzoefu wa mtu. Kutokana na Imani hii ya wajasiriamali juu ya kitu “makosa”, wemejifunza kitu kimoja cha muhimu katika biashara au maisha, nacho ni “kuyakiri makosa”. 

Kitendo cha kukiri makosa ndicho uwapa uwezo wa kusimama na kuanza tena pale inapotokea wakaanguka. Unapokubali kuwa makosa yametendeka na wewe pengine umehusika, ndipo akiri yako inafanyakazi katika viwango vya juu zaidi na hivyo kupata suruhisho la kudumu juu ya matatizo na changamoto zinazokukabili. 

Sasa ni wakati wa kufikiri juu ya maisha mazuri unayoyataka. Ni wakati wa chukua hatua (anza kufanya kwa vitendo), huku ukitambua kuwa makosa yatakuwa ni sehemu ya mchakato wa kufanya hicho unachofanya. Kila yatakapojitokeza makosa badala ya kutafuta mchawi, wewe yafungue makosa hayo, ili hatimaye uweze kunufaika na (masomo, ukweli na fursa)—yawezekana vyote hivi viko ndani ya mfuko wa makosa. Unatakiwa kuacha kulalamika, fungua mfuko wa makosa sasa na endelea kusonga mbele.


Jinsi ya Kuwa Mkubwa Kuliko Matatizo


“Utasonga mbele tu pale utakapoacha kujibinafsisha matatizo yanayoendelea kutokea katika mchakato wa maisha yako” ~ Cypridion Mushongi


Njia mojawapo ambayo ni kisababishi kikubwa cha hisia hasi na hasira ni hali ya kupenda kujibinafsisha au kujimilikisha matatizo yanayoendelea kutokea. Tabia au hali hii ya kupenda kujibinafsisha ni...
hatari kama ilivyobainishwa na bwana Ouspensky kwenye kitabu chake cha “In Search of the Miraculous: Fragments of an Unknown Teaching”(“nitumie kitabu”).

Hali hii ya kujibinafsisha matatizo, mara nyingi utokea pale unapochukulia jambo lililotokea kama la kwako binafsi au unalihusisha moja kwa moja na mtu au kitu fulani. Kila mara unaona matokeo ya matukio ya kuudhi au hali mbaya kama ya kwako binafsi. Wakati mwingine unaona matokeo ya matukio ya kuudhi kama mashambulizi dhidi ya kile unachokiamini wewe. Unajikuta unajihusisha kwa hisia zako zote na kujitambulisha na hali hiyo, kiasi kwamba inakuathiri kihisia, kifikra na kimtazamo katika hali ambayo ni hasi.

Walimu wakubwa katika masuala ya kidini, kama vile Buddha na Yesu, wamesistiza umuhimu wa kujitenganisha wewe na matukio yanayoendelea kutokea, ili kupata utulivu na kudhibiti hisia ulizonazo. 

Kwa upande mwingine mtaalam wa masuala ya saikolojia na falsafa bw. William James kutoka chuo kikuu cha Harvard (Marekani), aliwahi kuandika kuwa “hatua ya kwanza kwa tatizo au ugumu wowote ule ni kuwa tayari kulipokea kama lilivyo”. Pia mtaalam huyu aliwahamasisha watu kuwa kitu chochote ambacho hakiwezi kutibiwa lazima kivumiliwe. Kwa maneno mengine ni kwamba tunahitajika kujenga tabia ya kujitenganisha na mtu au hali ambayo inatufanya sisi kuwa na hasira au kuudhika. Inabidi tuondoe nguvu ya hisia zetu kwa mambo yanayotupa hasira, ili kupata utulivu na amani.

Njia hii haina maana kwamba ukubali kila kitu kibaya kinachokujia BADALA yake, inakuhamasisha kutumia nguvu yako ya akiri katika kudhibiti hisia hasi. Unajiwajibisha wewe binafsi kurudi nyuma kidogo na kukabiliana na matatizo au changamoto kwa akiri na busara zaidi. Unatumia akiri kuona hali halisi ilivyo na kufanya maamuzi mazuri ya kutatua tatizo lililopo. Hakuna watu wanaoweza kukudhibiti wewe labda kama kuna kitu fulani ambacho unahitaji kutoka kwao.

Lazima watu wengine wawe na kitu fulani ambacho bado wanaweza kukupatia au kuzuia usikipate. Mara moja utakapojitenga kihisia na mtu au kitu na ukawa hauhitaji chochote kutoka kwao, basi wewe huko huru. Hali hii ya kufanya mazoezi ya kujitenganisha na matukio au watu wanaokukwaza ni nguvu ambayo unaweza kuipata kwa kuijenga kupitia mazoezi ya kiakiri. Mazoezi haya yanaweza kukufanya ukawa mtaalam na bingwa wa kutatua matatizo yanayosababisha hasira.

Jambo moja unaloweza kulifanya ili kusaidia watu wengine, ni kuwatia moyo wao kuweza kujitenga na matukio ya matatizo na kutokushawishiwa na hisia katika kuliona na kulitatua tatizo. Wahamasishe, kuona ugumu na matatizo, kama vile yanatokea kwa wengine. Waulize ni ushauri gani wangeweza kutoa kwa mtu mwingine anayekabiliwa na tatizo kama hilo la kwao. Kwa kujitenga na hali inayotokana na hisia zilizoamshwa na tukio, wewe pamoja na wengine mtazidi kuwa na uwezo zaidi wa kutatua tatizo kwa ufanisi.

Kikubwa tunachojifunza hapa ni kwamba, wewe mtu binafsi ndiye mwenye uwezo wa kuamua ukubwa wa tatizo. Suala la tatizo kuwa kubwa au dogo ni la kihisia zaidi kuliko uhalisia. Na inaonekana kwamba matatizo tunayoyaita makubwa mengi ni yale tuliyosimuliwa na wakubwa zetu kuwa ni makubwa nasi tumeendelea kushikiria hisia hizo. Kwahiyo, inatupasa kila tukio tunalodhani ni tatizo kwetu tujenge utamaduni wakuwa tunalitafakari upya sisi kama sisi na tuliangalie na kulipima katika mazingira halisi ya wakati huo uliopo, ili kusudi tuweze kupata suruhisho lenye kuondoa tatizo lote kwa ujumla.

Ni muhimu sasa tutambue kuwa matatizo yataendelea kutokea kwa yeyote yule anayetaka na asiye taka, maskini na tajiri, aliyesoma na ambaye hakusoma, aliyejiajiri na aliyeajiriwa. Kitu cha msingi sana unachopaswa kukumbuka kila mara ni kwamba “wewe ni mkubwa sana kuliko matatizo uliyonayo”. Jambo la kushangaza ni kwamba watu wengi wameamua kuwa wadogo kuliko matatizo wanayokabiliana nayo na ndiyo maana wanajiona wana matatizo makubwa kuliko wenzao. Hali hii imesababisha watu wengi kukata tamaa ya maisha.

Mpendwa msomaji, yawezekana baada ya kusoma makala hii, umepata maswali mengi na pengine ungependelea kupata majibu na kuendelea kujifunza zaidi. 

Hivyo, napenda kukutaarifu kuwa bado unayo fursa ya kuwa mmojawapo wa kundi la wasomaji wa mtandao wa maarifashop: ni rahisi kwani unahitaji tu kuweka e-mail yako kwa kubonyeza neno “INGIA” . 

Ukimaliza kufanya hivyo, tayari wewe utakuwa na fursa ya kuwasiliana na mimi muda wowote na utaweza kupata makala, vitabu moja kwa moja kupitia e-mail yako kila mara vinapowekwa vitu vipya.

Pia unaweza kuniandikia au kupiga simu moja kwa moja ili kupata mafunzo mbalimbali kama vile uongozi wa biashara yako, kuifahamu pesa ni kitu gani, jinsi ya kutoka kwenye mkwamo kimaisha na mengine mengi yakiwemo ya jinsi ya kupambana na udhoofu wa mwili (afya na ustawi).

Fanya Mambo 5 Leo Kufaidi Nguvu ya Fikra Zako


Fikra zetu kutoka ndani ya akiri zetu ndiyo kila kitu. Fikra ndilo dirisha unalotumia kuangalia dunia na mambo yake yote. Ukishakuwa umelitabua hili utakubaliana na mimi kuwa unahitaji kuanza mara moja kujitathimini juu ya mwenendo wako. Unahitaji, kujenga na kuinua heshima yako juu na hii ikiwa ni pamoja na kupanua dirisha lako la fikra ili kuona zaidi fursa za mafanikio. 

Ili kupanua dirisha la fikra, inabidi kutunza  kujiamini na kujikinga dhidi ya athari zitokanazo na changamoto mabalimabali za kimaisha. 

Na hapa unahitaji kufahamu mambo 5 yatakayo kuwezesha kufanya uchunguzi wa undani ya fikra zako na hatimaye kupata msingi imara wa kuweza kuzijenga upya, ili ziwe katika mwelekeo ambao ni chanya. 

Ninatumaini kuwa, ukishakuwa umefahamu nini cha kufanya, basi utaweza kufahamu ni kitu gani unatakiwa kufanya na ni kwanini ni muhimu kwako.
Katika kuchunguza undani wa akiri yako na hatimaye kupanua dirisha lako la fikra zako, unahitaji kufikiria mambo 5 ya msingi:

1.      Jua Kuwa Maisha Yako, Yanatengenezwa na Fikra Unazozipa Kipaumbele Kila Siku.
Ukisoma kitabu cha Bwana James Allen kiitwacho “As a Man Thinketh” anatoa mafundisho ya kwamba, wewe binadamu ndiye unayetengeneza au kuharibu maisha yako mwenyewe kutokana na fikra juu ya fikra ulizonazo akirini mwako. Na pale unaporuhusu mawazo yatokee unakuwa ni muhanga wa maelfu ya mawazo hasi na imani finyu zinakuzunguka kupitia duara lenye taarifa hizo kila muda unaopita.

Unapokuwa mfikiriaji mahili wa mawazo (mtu mwenye kufikiri na kuchagua kile unachofikiria), basi jua kuwa hapo una uwezo wa kujenga maisha ambayo ni chanya na kutembea kila siku kuelekea kwenye ndoto yako ya maisha mazuri.

2.      Jua Kuwa Kubadili Kitu Chochote Nje ya Wewe, Lazima Ubadili Fikra Zako Kwanza.
Kama unataka watu wengine wabadili mtazamo wao wa jinsi wanavyochukulia au kukuona, lazima uanze kujibadili wewe kwanza. Kama unataka kubadili uchumi, jibadili wewe. Kama unataka kubadili hali ya maisha, jibadili wewe mwenyewe. Kama unataka kubadili dunia, jibadili wewe mwenyewe. Hiyo ndiyo kazi ya ndani yako ambayo utengeneza upenyo halisi na kuelekea kwenye mafanikio.

3.      Jua Kuwa Fikra Chanya Hazijengwi kwa Siku Moja.
Mwelekeo wa fikra ulizonazo ziwe chanya au hasi, zinajengwa ndani ya mzunguko wa siku 30. Baada ya siku 30 za kufanya kitu fulani, jua kwamba imekuwa tabia yako. Na maoni yako juu ya mwenendo wa maisha uliyonayo, pia ni matokeo ya tabia ya fikra zako za kila siku. 

Kwahiyo, usifanye kitu hiki siku ya Jumatatu peke yake na kutarajia kuwa millionia siku ya jumanne. Tambua kwamba ukiweka siku 30 za kufikiri mambo chanya fikra zako zitabadilika kwa kiasi kikubwa sana. Na baadae unapanda viwango kwenda hatua nyingine ya juu zaidi na kuendelea…

4.      Jua Kuwa Unatengeneza Maisha Mazuri kwa Kujenga Taswira Nzuri Mwenyewe.
Taswira yako inatengenezwa na picha ya iliyoko kwenye ubongo na ambayo inachezesha fikra zako kwa siku nzima. Ni jinsi gani unavyojiona wewe mwenyewe kufanikiwa au kutofanikiwa. Ndiyo sababu, jambo namba moja hapo juu ni muhimu sana.

5.      Jua Kuwa Kile Unachokiamini Ndicho Kinawezekana
Kama kweli unaamini unaweza kufanya chochote na ukafanyia kazi imani hiyo, basi kwa hakika utaweza kufanikisha ndoto yako. Ni lazima uamini kuwa unaweza kufanya kitu chochote. Unaweza kuimba kwamba “unaaamini unaweza kupaa,” lakini hauamini kwamba unaweza kufanya hivyo na kwahiyo, sheria ya uvutano bado inafanya kazi. 

Na inaweza kuwa kukuhamasisha ukajikuta unapendekeza kuwa unaweza kusogeza mlima kwa kutumia mbegu ya ndogo sana ya zao la ulezi, lakini wote tunajua kuwa hicho ni kitu ambacho hakiwezi kutokea. Lakini unapokuwa umeweka malengo, unaweza kwa dhati ukayatimiza kwa kwenda kuyafanyia kazi, na ikawezekana kuwa hivyo. Hakikisha kuwa unafanya kazi na kutimiza majukumu yako ya kila siku yanayohusu maendeleo yako binafsi.

Jitahidi kuweka fikra chanya na kujua kwamba sehemu yako ya ubongo inayoitwa subconscious itakuongoza wewe kuchukua hatua moja baada ya nyingine hadi kufanikisha hicho ulichokipanga kukifanya kuwa dhahiri. Endapo utakuwa umenielewa nazungumzia nini juu kuchukua hatua dhidi ya ya mambo 5 hapo juu, basi hapana shaka unaweza kuishi ndoto zako. Na hiki ndicho ninachokutakia ukifanye.





AMUA KUWA RAIS WA MAISHA YAKO LEO
Maisha unayoishi sasa ni maisha yako, kama kuna sehemu yoyote ya maisha yako ambayo huipendi wewe ndio una jukumu la kuibadilisha. Hakuna mtu mwingine yeyote ambaye anaweza kuwa na uchungu na maisha yako ila wewe mwenyewe. Na wala hakuna mtu yeyote anayeweza kuyabadili maisha yako bila yaw ewe mwenyewe kuwa tayari kwa mabadiliko.

Kuanzia sasa jichukulie wewe kama raisi wa maisha yako, na jichukulie wewe ndio mtu wa mwisho wa kufanya maamuzi juu ya maisha yako. Na sio tu unajichukulia hivi, bali ndio ukweli wenyewe. Wewe kama raisi maamuzi yako yanaweza kusababisha mafanikio au yakasababisha kushindwa. Kama tulivyoona kwenye siku ya kwanza upo hapo ulipo kutokana na maamuzi uliyofanya na machaguo uliyofanya. Ili kwenda mbele zaidi unahitaji kufanya maamuzi bora zaidi na kuboresha machaguo yako.

Miasha ni kuchagua, ukichagua kufanikiwa ndiyo utakachokipata, ukichagua kuwa wa matatizo na kushindwa ndicho kitakachotokea. Usipochagua kabisa utapata kile kilicho kibovu kabisa ambacho ni kushindwa. Kipato unachopata leo ndio kipato ulichoamua kupokea, kama kipato unachopata sasa hakikuridhishi amua kupata zaidi ya hapo. Fanya hilo kama lengo lako, weka mipango na anza kufanyia kazi mpango wako wa kujiongezea kipato. Ukikaa tu na kulalamika kwamba kipato hakikutoshi huku hufanyi chochote cha kukiongeza unapoteza muda wako.

Wewe ndio raisi wa maisha yako, wewe ndio mfanya maamuzi mkuu na wewe ndio unayetengeneza maisha yako. Kama utakuwa na mtizamo hasi utajenga maisha ya matatizo na kushindwa na kama ukiwa na mtizamo chanya wa kuona unaweza kubadili maisha yako utatengeneza maisha ya mafanikio na furaha. Yote haya yapo mikononi mwako ni wewe tu ufanye maamuzi sahihi na kuyasimamia.
~ TWENDE KAZI PAMOJA ~

2 comments:

Unknown said...

Nakubaliana nawe kuwa lazima uwe raisi wa maisha yako ili utawala uendelee na hatimaye ufanikiwe kweli

MUSHONGI said...

Tatizo letu wengi tunachelewa kuchukua hatua kwasababu ya kasumba ya kufikiri kuwa viongozi ni wale wa kisiasa tu ndio maana ata mkuu wa kaya anasubili mkuu wa wilaya amwambie kuwa ni muhimu kuweka akiba ya chakula; Dereva wa basi anaendesha gari kwa mwendo kasi naye anasubili abiria wa mwambie ni hatari. Ndugu hapo ndo tulipo Tanzania uijuavyo.