Sunday, May 31, 2015

Bila Picha Mpya Hakuna Jipya



·        Watu wengi wanafikiri kwa kutumia vitu vilivyopo tu!
·        Picha ya maisha mazuri haipo kwenye akili ya walio wengi!

Maendeleo yaliyopo kwa sasa yametokana na mawazo pamoja na picha mbalimbali zilizojengeka ndani ya ubongo wa binadamu. Vitu vyote tunaviona ambavyo vimetengenezwa na binadamu, vilitokana na mawazo na taswira/picha zilizoumbwa ndani ya ubongo wa mtu. Baada ya kuumba picha au taswira ya kile kinachohitajika kufanyika ndipo binadamu huweza kutumia nyenzo mbalimbali pamoja na malighafi nyinginezo kutengeneza vitu halisi, huku akiongozwa na ile taswira iliyoko kwenye akili ndani ya ubongo wake.

Nyumba ni mfano mmojawapo wa vitu halisi ambavyo huanza kama wazo. Leo hii tuna nyumba za kila aina, kwasababu mara nyingi tuna wasanifu majengo ambao kila mara uanza nyumba kwa kufikiria jinsi itakavyokuwa hata kama haijajengwa na baadae uchora ramani yake ambayo wajenzi uitumia katika kusimamisha jengo. Kwahiyo, aina mbalimbali za majumba tunazoziona leo zilitokana na fikra na ujenzi wa taswira ndani ya ubongo wa watu hao ambao ni wasanifu majengo (architect). Nyumba ikishakamilika ndipo watu wengine hupata fursa ya kujua kilichokuwa akilini mwa huyo mtu na pindi watoto wanapozaliwa na kukua ujenga mawazo na taswira ya kurithi kutokana na vitu vilivyopo tayari. Kwahiyo, mtoto akikua na kufikia wakati wa kujenga nyumba yake, moja kwa moja anapata picha ya nyumba kwenye ubongo wake ambayo ni ya kurithi kutoka kwenye nyumba zilizojengwa tayari. Kwa namna moja au nyingine ile picha iliyobuniwa kwenye ubongo wa mtu wa kwanza anakuwa ameinakiri kutoka nyumba halisi na kuijenga mara ya pili.

Katika nchi nyingi ikiwemo Tanzania, ambazo hazijapiga hatua kubwa kimaendeleo; vitu vingi vinavyofanyika vimetokana na taswira ya vitu halisi ambavyo tayari vipo na vinaonekana. Imejengeka tabia ya watu walio wengi kuhoji hasa pale mtu Fulani anapojaribu kuibua jambo jipya, mara nyingi linakataliwa eti! Kwa kisingizio cha kwamba “halijawahi kufanyika popote”. Kwahiyo, watu wanajisikia amani zaidi wanapoona wanafanya kitu ambacho tayari kinafanyika kwingine. Hali ya namna hii ndiyo inaendelea kutufanya tuendelee kuwa wategemezi na ombaoma mbele ya jamii ya kimataifa. Utamaduni huu wa kuendelea kutumia uzoefu na kuzama kwenye vitu vilivyoko mbele yetu muda wote (hali halisi), ndio unaotusababishia kuendelea kupata changamoto, matatizo na uzoefu ule ule miaka nenda rudi!. Mara nyingi uzoefu na elimu juu ya jambo fulani, ni vitu ambavyo vimejengeka kutokana na mambo yaliyopita au vitu vya zamani, kiasi kwamba, wewe unachofanya ni kuvikariri na kuvitoa upya, hali ambayo kiukweli kunakuwa hakuna jipya lolote la kutokea.

Misuli ya kuwaza ndani ya ubongo wetu, ndiyo hubadilisha mawazo na fikra zetu kuwa vitu kamili. Picha na fikra juu ya kitu tukitakacho, ndivyo vitu muhimu vinavyohitajika katika kujenga maisha mazuri ya baadae. Ni kwakutumia picha iliyoumbika ndani ya ubongo wetu, ndipo tunaweza kuona jinsi tunavyotaka maisha yetu ya baadae yawe. Tukishakuwa tumeyaona maisha mazuri ndani ya ubongo wetu, ndipo tunaweza kupata hari na shauku kubwa ya kuyatafuta hayo maisha ya ndoto yetu. Kwahiyo, ni wakati muhafaka sasa kwa kila mtanzania kujenga tabia ya ubunifu na kuendelea kujikita katika kufikiri mambo mapya na vitu vingine nje ya hivi vilivyopo. Kila mtu aanze kwa kutengeneza picha ndani ya ubongo wake juu ya maisha mazuri anayoyatamani na baadae kuweka mikakati ikifuatiwa na utekelezaji. Iwapo tutaweza kupata picha ya maisha tuyatakayo na jinsi tunavyopenda yawe, basi nguvu kubwa itakuwa imewekwa kwenye mwendo na mabadiliko makubwa  yakiambatana na maisha mazuri yatatokea bila pingamizi lolote. Kumbuka kuwa asilimia 80% ya mafanikio yako yataletwa na wewe mwenyewe na asilimia 20%  ndiyo inategemea watu wengine.

Mpendwa msomaji, endelea kuitumia vizuri MAARIFASHOP ili kujifunza mambo mbalimbali yatakayokuwezesha kupata mafanikio. Ili kupata makala mpya kila zinapochapishwa, bonyeza neno TUMA MAKALA MAARIFASHOP kisha sajiri barua pepe yako. Na kama unapenda kupata mafunzo ya kila siku kwa njia ya whatsap bonyeza neno MAFUNZO

Kazi ni kwako! Timiza wajibu wako!

Sunday, May 24, 2015

Ajira Siyo Kazi ni Ajira na Kazi Siyo Ajira ni Kazi

Sasa hivi kuna tatizo kubwa sana la ukosefu wa ajira hasa kwa vijana. Ukosefu wa ajira ni jambo ambalo linazidi kuwawangisha  vichwa wadau wengi wa maendeleo na hasa serikali. Ni kweli serikali ina jukumu la kuhakikisha wananchi wake wanakuwa na shughuli ya kufanya ili kujiongezea kipato. Lakini, wakati jitihada za serikali zikiendelea, sisi wenyewe tunaodai kukosa kazi tunayo majukumu makubwa zaidi ya kufanya kuliko kutegemea watu wakutupatia ajira. Kwahiyo, ni vyema tushughulikie kwanza yale yote yaliyondani ya uwezo wetu ambayo nina imani yanaweza kuchagia kwa asilimia 80% katika kutupatia suruhisho la kudumu juu ya kero hii ya kukosa kazi. Hivyo basi, hatua ya kwanza kabisa ni kutafakari na kufikiri kwa kina juu ya tofauti iliyopo kati ya kazi na ajira. Maana unaweza kujikuta muda wako mwingi unautumia kutafuta ajira ukifikiri ni “Kazi”.

Kazi na ajira ni vitu viwili tofauti kabisa, na haviwezi kulinganishwa kwa kiwango chochote kile. Kazi inalipa sana na malipo yake mengine hayana kikomo, tofauti na ajira ambayo malipo yake ni kidogo na yanaweza kukoma muda wowote. Kitu cha ajabu kabisa ni kwamba watu wengi wanapendelea “ajira” kuliko “kazi” kwasababu, ulipohitimu elimu yako ulikaririshwa kuwa kazi inayotambulika rasimi ni ajira. Hii inatokana na mazoea ambayo tumeyajenga tokea tukiwa wadogo kuwa kazi yenye heshima ni ambayo umeajiriwa, ndiyo maana wale wote wanaofanya shughuli za kuajiriwa eti! ndio wanaitwa “Wafanyakazi”. Kwahiyo, wale wote ambao hawana ajira na hasa ajira rasimi, wanajiona na kujisikia kuwa hawana kazi na kutafuta njia usiku na mchana ili angalau siku moja waweze kuajiriwa. Hali hii, ya kushindwa kupata majibu sahii juu ya kazi ni ipi na ajira ni ipi. Matokeo yake kumeibuka makundi mawili ambayo ni kundi la wenye jukumu la kutoa ajira na kundi jingine ni la wenye kupata ajira. Kundi la wapata ajira ni wengi sana; Eti! Kazi yao ni kutafuta wapi ajira ilipo, na pale mtu anapotafuta ajira akakosa kwa muda huo, moja kwa moja anasema sina kazi! Hii inashangaza sana.

“Ajira” ni kufanya kazi ambayo siyo ya kwako, waweza kuwa unaipenda au huipendi. Watu wengine hawapendi kazi walizoajiriwa kuzifanya, lakini yawezekana  wanaendelea kufanya kazi hizo kwasababu wanalipwa pesa. Kutokana na hali hii, watu wengi hulazimika kutafuta kazi nyingine pale tu malipo yanapokuwa hayatoshelezi mahitaji ya muhusika. Mwenye kazi “mwajiri” anapokuwa amekuajiri kwenye kazi yake ambayo “siyo ya kwako”; wewe moja kwa moja unahesabika kuwa ni sehemu ya gharama za uendeshaji wa kazi au kampuni! Hii ni sawa na kusema kuwa waajiri wengi wanawaona wafanyakazi (waajiriwa) kama gharama za uzalishaji!. Hii haina maana kwamba waajiri hawawathamini waajiriwa wao, bali wakati wa kufanya tathimini ya maendeleo ya kazi inawabidi kufanya hivyo, ili kupanga mipango mikakati ya kuwezesha matunda ya kazi husika yapatikane kwa gharama nafuu.

 “Kazi” ni majumuisho ya majukumu mbalimbali ambayo kwa mwenye kazi unajiwajibisha mwenyewe katika kuyatimiza hayo uliyojipa mwenyewe, bila kutegemea kulipwa chochote mpaka matunda ya kazi hiyo yapatikane. Unapofanya kazi siyo lazima alipwe, kwasababu mara nyingi kazi inakuwa ni mchakato wako wa maisha na haupangiwi na mtu yeyote, wewe mwenyewe unajipangia ni nini ufanye, kwa malengo yapi na ni nani unamlenga kunufaika na matokeo (matunda) ya kazi yako. Iwapo matokeo ya kazi yako yanatoa suluhisho la matatizo au kero zilizopo kwenye jamii husika, basi ujiandae kulipwa malipo ambayo hayana kikomo, kwasababu watu watanunua matunda ya kazi yako, ili kukidhi mahitaji yao, hivyo ni rahisi wewe kuweza kutajirika kutajirika kupitia utatuzi wa kero na matatizo mbalimbali. 

 Kutokana na maana pana ya “kazi” tunaona kwamba kazi inaweza kupatikana popote lakini ajira haipatikani kila sehemu. Kazi ni nyingi sana ajira ni chache sana, hii inamanisha kwamba watu wanapenda vitu ambavyo vimeishapikwa tayari, kazi yao ni kupakua na isitoshe hata kwa kupakua tu! unalipwa na mwenye kazi. Kazi ni ya kudumu wakati ajira ina ukomo; kwenye kazi hakuna bosi, isipokuwa bosi wako ni malengo na ndoto zako lakini kwenye ajira kuna bosi ambaye anayo madaraka ya kuamua juu ya nini kifanyike na wakati mwingine kifanyike vipi na huyu ndiye anamiliki na kuongoza hatima ya mafanikio yako
na hasa ya kiuchumi. Kwenye kazi unachukua muda mrefu kuanza kulipwa tofauti na ajira ambayo, ukianza tu ajira yako unaanza kulipwa maramoja au mwisho wa mwezi huo huo. Pengine tofauti hii ya muda wa kulipwa kati ya mwenye kazi na mwenye ajira ndiyo inayowafanya watu wengi na hasa wasomi wa fani mbalimbali kupendela “ajira” kuliko “kazi”.

Kutengeneza na kufanya kazi kunahitaji kujitoa, ubunifu, kufikiri sana, kuvumilia na zaidi ya yote, kazi inahitai ujasiri na ninadhani ujasiri huu wa kufanya kazi bila kulipwa kwa wakati huo ndiyo mzizi mkuu wa neno “Ujasiriamali”. Kwenye ajira kila kitu ambacho unakifanya unadai ulipwe, kwahiyo, kama hakuna malipo hicho kitu au shughuli haiwezi kufanyika. Kwa uhalisia ni haki ya mwajiliwa kudai malipo ya kila nguvu anayowekeza kwenye ajira yake kwasababu, mwajiriwa kama mwajiriwa yeye hana umiliki wowote wala hisa juu ya matokeo au mapato yote ya  kile kilichozalishwa bali mwenye kumiliki hicho ni mwenye kazi. Waajiriwa hupewa sehemu ndogo sana ya kile chote kilichozalishwa. Makampuni mengi, kila mwisho wa mwaka huwa wanafunga mahesabu na kupima wamepata faida kiasi gani lakini siyo rahisi kwa mwenye kampuni kutoa gawio (dividend) kwa wafanyakazi wake kwasababu, wafanyakazi (waajiriwa) wote, wanahesabika kama sehemu ya gharama na siyo sehemu ya faida, na faida hii ndiyo motisha na kichocheo kikubwa cha yeye kuendelea kuwekeza na kutengeneza kazi nyingi ambazo zinaweza kutoa ajira kwa watu wengi zaidi. 

Kwakuwa kazi unajipatia mwenyewe, ni wakati muhafaka sasa wa kujipa kazi badala ya kusubili kupewa kazi (ajira). Tusisubili wale wakutuletea kazi, kwa maana hatujui wataleta lini na kwa malengo yapi. Tuzidi kukumbuka kuwa ajira haziwezi kuwa nyingi kama kazi zinazotengenezwa ni chache. Tuzidi kujipa kazi kwani chochote tutakachozalisha, watu wako tayari kununua, ilimradi kina manufaa kwao. Anza leo, kuanza kujitenga na watafuta ajira, pia jiepushe na tabia ya kulalamikia watu wengine kwa mambo ambayo ni majukumu yako. Kwahiyo, bila kujali umesomea nini, anza leo kufikiria ni kitu gani unaweza kukizalisha ambacho kina uwezo wa kutatua kero na changamoto mbalimbali katika jamii. Kwakufanya hivyo, utakuwa umepata suluhisho la kudumu juu ya kero ya muda mrefu ambayo ni ukosefu wakazi”.

Mpendwa msomaji, endelea kuitumia vizuri MAARIFASHOP ili kujifunza mambo mbalimbali yatakayokuwezesha kupata mafanikio. Ili kupata makala mpya kila zinapochapishwa, bonyeza neno TUMA MAKALA MAARIFASHOP kisha sajiri barua pepe yako. Na kama unapenda kupata mafunzo ya kila siku kwa njia ya whatsap bonyeza neno MAFUNZO

Sunday, May 17, 2015

Watu Hawajui Kitu Wanachohitaji Kama Hawajakiona Ongeza Kasi ya Ubunifu Soko Lipo

Mara zote tunapenda kuhitaji bidhaa ambazo tayari tumeziona zipo au tumezizoea. Utafiti umebaini kuwa mahitaji ya binadamu huwa hayana kikomo, kiasi kwamba kila mara anhitaji ama kitu kipya au kile alichokizoea. Ukweli ni kwamba, bado maisha yetu ni magumu kwasababu bado tunatumia nguvu nyingi kufanikisha mambo mbalimbali yanayohitajika katika maisha yetu kwa ujumla. Ugumu wa maisha unatokana na kiwango kidogo sana cha ubunifu na uzalishaji wa bidhaa. Hapa Tanzania, bado tunazidi kutegemea mbinu zile zile za zamani ambazo wazee wetu walizitumia wakati huo kupambana na maisha. Maana yake ni kwamba katika zama hizi hatujatoa jipya sana lenye kuendana na kasi ya mabadiliko yanayoendelea kutokea duniani kote.

Kwa sasa Tanzania, tuna mahitaji makubwa sana ya ubunifu na teknolojia katika nyanja mbalimbali za maisha. Yawezekana watu wengine wako tayari kulifanya hili lakini wanaogopa au wana hofu na mashaka juu ya kukosekana kwa soko la bidhaa mpya ambazo zitatokana na ubunifu au teknolojia mpya. Kamahiyo, kama hiyo ni mojawapo ya sababu, basi tunatakiwa kuondoa hofu na kuanza kufikiria “tutaipatia nini dunia”, yaani tuwe na mtazamo kama wa watu wa sanaa (craftsman mindset).  Watu katika fani ya sanaa ni mfano wa kuigwa, kwani wao huwa hawasubili watu wawambie nini wanataka, bali wao uchukua muda wao na kuwaza ni kitu gani kinaweza kuwafurahisha watu basi! na kweli kama ni mziki ukitoka, unaona kila mmoja anajaribu kusaka CD ili kununua.

Hapa Tanzania, katika kipindi cha miaka kumi iliyopita kuna vitu vimeibuliwa ambavyo havikuwepo huko nyuma. Lakini baada ya wabunifu mbalimbali kuvileta kwetu, tumejikuta tunavihitaji sana kiasi cha kwamba, kuna watu wengi ambao hawawezi kufanya mambo yao yakaenda sawasawa bila kutumia vitu hivyo. Mifano ni mingi sana, lakini tuangalie michache tu kama ya usafiri wa pikipiki, chakula cha ndizi na matumizi ya simu za mkononi

Usafiri wa pikipiki: Huduma ambayo haikuwepo huko nyuma hii ya usafiri wa pikipiki maarufu kama “BODA BODA”. Ebu jiulize kabla ya ujio wa usafiri huu, watu walikuwa wanatumia nini kusafiri? Najua utasema magari, lakini walio wengi, magari yalikuwa hayawezi kufika majumbani kwao. Kwa wale wanaofanya kazi hasa sehemu za starehe, wanalazimika kutoka kazini wakati wa usiku wa manane, usafiri huu wa pikipiki umekuwa mkombozi kwao. Kumbe kwa muda wote ambao hakukuwepo na usafiri wa pikipiki, watu waliendelea na maisha kama kawaida na kwa wakati huo hakuna  aliyewahi kufikiria juu ya mahitaji makubwa ya usafiri huu. Kwa maana nyingine ni kwamba, tangu zamani tulikuwa na mahitaji makubwa ya huduma hii, lakini hatukujua kabisa kama tulihitaji kitu hicho, mpaka kilivyoletwa na wabunifu wetu, ndio tukaanza kujisikia kuwa na mahitaji ya Usafiri wa pikipiki.

Chakula cha ndizi: Hapo zamani tulikuwa na makundi manne ya ndizi (kupika, mbivu, kuchoma/kukaanga na pombe). Aina ambazo zilikuwa kwenye kundi la ndizi za kuchoma na kukaanga, kwa hapa Bukoba zinafahamika kama “e’nkonjwa/gonja” na huko Karagwe ni “e’ngarambi”. Kutokana na matatizo mbalimbali, aina hii ya ndizi ilianza kupungua na hivyo kuadimika. Kutokana na kuadimika kwake, ndipo wajasiriamali hasa kutokea miji ya kanda ya ziwa,  walipoamua kujaribu kukaanga aina nyingine kutoka kundi la ndizi za kupika, lengo likiwa ni kuhakikisha wanawapatia wateja wao angalau ndizi wakati wanapo kula nyama choma. Baada ya watu kuonja aina nyingine ya ndizi hizi za kupika, walitokea kuzipenda pia na ndipo mahitaji ya ndizi za kupika yakaongezeka mara mbili yaani zikawa zinakaangwa na wakati huhuo zikawa zina pikwa. Hivyo, tunaona kwamba watu kwa sasa wanahitaji sana ndizi zilizokaangwa bila kujali ni aina ipi ya ndizi, japo wakipata ile ya aina ya “gonja” wanafurahi zaidi. Watoto waliozaliwa hivi karibuni na kukulia kanda ya ziwa hawatajua kuwa kulikuwa na aina fulani ya ndizi ambayo ni maalumu kwaajili ya kukaanga, bali watapokea kilichopo au kitakachokuja baadae na hicho ndicho watazidi kuhitaji.


Matumizi ya simu za mkononi: Tualiowengi hawakujua kama wanahitaji mawasiliano ili kuweza kufanya biashara na shughuli nyingine za kimaisha. Wale wagumu walianza kuwasema wenzao kwamba wanapoteza pesa kwa kupiga simu lakini kwakuwa simu tayari zilianza kuonekana kila mahali basi na wale waliofikiri kuwa hawazihitaji baadae waliona umuhimu wa simu. Baada ya watu wengi kumiliki simu za mkononi, sasa kuna aina mpya zijulikanazo kama “Smartphone” aina hizi za simu kwa Kagera zinajulikana kwa jina maarufu kama “tachi”. Tunaona kuwa kadiri siku zinavyokwenda watu wengi wanazidi kuona umuhimu wa simu za aina hii, kwasababu wale ambao hawajaamua kuwa nazo, wanaona wenzao wenye simu hizo wanavyofaidika na Huduma zipatikanazo kwenye simu za “Smartphone”. Mfano: wale wenye magari wanaweza kupiga picha spare na vipuli vya aina mbalimbali na kuvituma kwa wenye maduka ili kujua kama vinapatikana na ni bei gani, wengine wanaweza kupata taarifa kwa picha juu ya aina za nguo na mitindo mbalimbali n.k. Tokea huko nyuma hatukujua kama tulihitaji huduma za namna hii kwasababu tulikuwa hatujaziona, lakini baada ya kuona umuhimu wa matumizi ya simu, sasa tuna mahitaji makubwa sana.

Kwakuwa watu wanapenda kuona kitu kwanza alafu ndio wanahitaji, basi hali hii inatoa fursa ya kufanikiwa haraka kwa wale wote ambao wako tayari kufikiri, kubuni na kugundua vitu vipya, kwasababu, soko lipo la kutosha kwa wazalishaji wote. Kinachotakiwa ni kwamba kitu kipya ulicholeta kiwe na manufaa makubwa kwa watu waliowengi. Ni muhimu kwa wapenda mafanikio kukaa muda wote katika hali ya utafiti kwenye jamii. Kwakufanya hivyo, ndipo tutaweza kugundua mahitaji muhimu ambayo ni mapya. 


Ili kufanikisha hili, ni vyema tukajifunza jinsi ya kutumia macho ya ubongo kuona fursa badala ya kutumia macho ya kawaida kama tulivyozoea. Pia, tunahitaji kuwekeza muda mwingi kufikiri na kuchambua hali ya maisha yetu na tunatakiwa kuwa wadadisi kila mahali tunapokuwa, na hatimaye tuchukue hatua na kuanza kuzalisha bidhaa mpya na zenye manufaa makubwa kwa jamii. 

Wito kwa wajasiriamali; ni muhimu sana tuanze sasa kutumia muda mwingi tulionao kufikiri na kuongeza kasi ya ubunifu katika kila nyanja ya maisha. Likifanyika hili, tuna uhakika wa kupiga hatua kubwa sana kimaendeleo hasa ya kiuchumi na kijamii. Wito pia ni kwa wale wote waliokabidhiwa majukumu ya kuweka mazingira wezeshi kuendelea kulisimamia hili, kwani tunaanza kuona ongezeko la vijana ambao wako tayari kufikiri na kubuni vitu vipya ambavyo hatimaye vitarahisisha maisha na hivyo kuendelea kuifanya Tanzania kuwa mahali pazuri pa kuishi.

Mpendwa msomaji, endelea kuitumia vizuri MAARIFASHOP ili kujifunza mambo mbalimbali yatakayokuwezesha kupata mafanikio. Ili kupata makala mpya kila zinapochapishwa, bonyeza neno TUMA MAKALA MAARIFASHOP kisha sajiri barua pepe yako. Na kama unapenda kupata mafunzo ya kila siku kwa njia ya whatsap bonyeza neno MAFUNZO

Tuesday, May 12, 2015

Usibane Matumizi ya Kipato Tumia Kipato Kupanua Njia za Kuingiza Kipato




Yawezekana unaendelea kuishi maisha duni, kwasababu unaishi kwa “kubana matumizi”; na hii ni kutokana na ukweli kwamba, tangu tukiwa wadogo tumefundishwa na wazazi, ndugu jamaa na marafiki kuwa ili uweze kuwa salama ni “Ishi Chini ya Uwezo Wako”. Watu wengi wenye mtazamo huu, mara nyingi wanaotumia njia ya kubana matumizi kuwa ndiyo suluhisho na njia pekee ya kukabiliana na ugumu wa  wa maisha. Ukweli ni kwamba, kubana matumizi ni utaratibu mzuri lakini inategemea una malengo gani ya kufanya hivyo. Kutokana na kutotambua ubaya wa tabia ya kubana matumizi, wengi wamelichukulia kuwa ni utaratibu wa kudumu badala ya kuwa wa muda tu!. 

Watu wameendelea kubana matumizi tangu wanajitabua mpaka wanazeeka. Unapokuwa mtu wa “kubana matumizi” muda wote, kinachojitokeza ni kwamba unajenga hofu kubwa ndani yako juu ya kuishiwa pesa kidogo uliyonayo. Akiri yako yote inaelekezwa kulinda pesa yako isitoke au wengine wanasema eti! Itoke kwa mpangilio – lakini mwisho wa yote hali inabakia palepale “kuishiwa na kutaabika”. Kwa mtu ambaye amejiwekea utaratibu wa kudumu wa kubana matumizi, akiri yake inadumaa sana kiasi cha kukubali kuishi maisha duni na ufukara. Mtu wa namna hii kila anapotafuta na kupata, badala ya kuwaza ni kwa namna gani atapata kingi zaidi, yeye mara moja unawazia kuishiwa, ndiyo maana anaanza kuweka nguvu nyingi kubana hicho kidogo kilichopatikana. Mwisho anatumia kwa kujinyima sana na hatimaye kinaisha ndipo huyo mtu uhanza tena kutafuta. Kwahiyo, unajikuta umenasa katika mzunguko wa kuishiwa na maisha yanakuwa ni ya kubangaiza miaka yote. 

Kuishi chini ya uwezo wako ni kitu cha kawaida na mara nyingi ushauri utolewa sana na wataalam na wasomi wa masuala ya biashara na uchumi kuwa njia pekee ya kuendana na hali ni kufanya vitu vilivyo chini ya au vinanavyolingana na uwezo wako. Lakini badala ya kulikubali hili bila kulitafakali ngoja tujiulize ni kwanini wanasema hivi? Au kwanini imani hii ya kubana matumizi inatokea? chimbuko la kubana matumizi ni kuazia wakati ule wa zama za kale ambapo binadamu aliishi kwa kukusanya matunda na kuwinda wanyama. Wakati huo, watu hawakuwa na fikra za uzalishaji, kwasababu walizoea kula vitu ambavyo vilijiotea na kukua vyenyewe bila kutegemea akiri na nguvu ya binadamu. 

Kazi ya binadamu wakati huo ilikuwa ni kutafuta na pale vilipopatikana vilikusanywa kiasi cha kutosha. Baada ya kuvikusanya, binadamu huyo wa kale alijitahidi sana kuvitunza ili vikae muda mrefu bila kuisha. Kwakuwa vitu hivi mara nyingi vilikuwa vinatoka mbali sana na makazi yao, ilibidi kujitahidi kubana ili kupunguza safari za kwenda huko; njiani walipambana na wanyama wakali, mafuriko, mvua n.k. kwahiyo kila walikuwa wakifkiria safari ilikuwa ni budi wabane kupunguza hadha za namna hiyo. Sasa wewe unayeishi katika zama hizi za leo, tayari una uwezo wa kuzalisha bidhaa na huduma mbalimbali, na hivyo kutotarajiwa kuishi kwa style kama ya enzi za kale. Uhamuzi ni wako kwa maana kwamba unaweza kuamua kuzalisha vingi na ukatumia kiasi unachoona kinafaa kukutoshereza mahitaj yako ya wakati huo. Badala ya kila wakati kufikiria kubana matumizi na mwisho kuishia kuishi katika maisha ya kupata mahitaji chini ya kiwango chako halisi. 

Kuishi chini ya uwezo wako ni sawa a kujiaminisha kuwa suluhisho la kumudu gharama za maisha ni kupunguza matumizi. Kuishi juu ya uwezo wako ni sawa na kujiaminisha kuwa pesa ipo nyingi. Hali zote mbili hazifai, bali suluhisho pekee ni kupanua na kuongeza vyanzo vya mapato. Kila mmoja anaweza kupunguza matumizi, na kila mmoja anaweza kutumaini na kuomba Mungu kuwa pesa itakuja, lakini inahitaji ubunifu, maarifa na uelewa, pamoja na ujasiri ili kukuza na kupanua mapato yako kupitia njia halali. Kimsingi siamini katika kuishi chini ya uwezo na wala kuishi juu ya uwezo, ninachoamini ni kuishi kwa kupanua na kuongeza njia za kuleta mapato. 

Siamini katika mtazamo wa “ishi chini ya uwezo wako”; kwa ujumla mtazamo huu ni wa kimaskini na siyo mzuri. Lakini pia, kibaya zaidi ni kwamba ushauri huu wa kuishi chini ya uwezo unasababisha kuua kabisa dhamira na fikra za ujasiriamali. Ushauri huu unakufanya usinyae kuwa mdogo. Hali hii inafanya mtu anakuwa na maisha duni kuliko alivyopaswa kuwa. Hali hii pia inakufanya kuingia katika kundi la watu wa kawaida au wenye mawazo ya wastani (mediocre). Na kama uliwahi kuambiwa na wewe mwenyewe kuwazia kwamba unatakiwa kuishi chini ya uwezo wako acha mara moja. Huu ni wakati wa kukua na kufanya mambo makubwa, ni wakati wa kuwekeza asilimia kubwa ya kipato chako kwenye vitu vinavyoingiza pesa kwako; ni wakati wa kuwa mbunifu na kupanua siyo tu njia za kuingiza kipato, bali pia jitanue kwa kuilisha akili yako ili uweze kufaidika na fursa zilizokuzunguka.

Mpendwa msomaji, endelea kuitumia vizuri MAARIFASHOP ili kujifunza mambo mbalimbali yatakayokuwezesha kupata mafanikio. Ili kupata makala mpya kila zinapochapishwa, bonyeza neno TUMA MAKALA MAARIFASHOP kisha sajiri barua pepe yako. Na kama unapenda kupata mafunzo ya kila siku kwa njia ya whatsap bonyeza neno MAFUNZO

Monday, May 4, 2015

Shule ya “Maisha Yako” Inataka Malengo na Mipangilio Yako Iwe ni kwa Maandishi


Kumbukumbu ni kitu muhimu sana katika kujenga misingi imara ya mafanikio yoyote yale. Watu tuna kumbukmbu nyingi na za kila  aina ndani ya vichwa vetu. Kutokana na hazina hii ya kumbukumbu, watu wengi uzitegemea sana katika kufanya maamuzi ya shughuli mbalimbali za kila siku. Lakini, utafiti umebaini kuwa, huwezi kupata mafanikio makubwa ambayo ni endelevu, kama huna ndoto ya aina ya maisha unayoyataka. Kwa walio wengi yawezekana wana ndoto kubwa, lakini ndoto hizo hazitimii kwasababu mbalimbali, na sababu mojawapo ambayo ni muhimu ni kuendekeza utamaduni na tabia ya kutekeleza mipango kutokea kichwani.

Kumbuka kuwa, kila siku ubongo wetu unapokea na kutunza kumbukumbu nyingi sana, kiasi kwamba, inakuwa vigumu kwako wewe kuweza kukumbuka mambo muhimu ambayo unahitaji kuyatimiza. Matokeo yake, unajikuta kila siku unashughulika na vitu vipya tu! Au kulingana na mambo yanavyojitokeza. Mara nyingi shughuli zako zilizo nyingi zinakuwa hazina mwendelezo wa pamoja. Hii ni hatari sana kwa mafanikio na pia, ni vizuri ukafahamu kuwa, kuendelea kukumbatia tabia hii ya kutegemea kumbukumbu ambazo ziko kichwani, itakuwa ni vigumu sana kufikia maisha ya ndoto yako.

Tunapoongelea kumbukumbu hatuamanishi zile za mapato na matumizi tu! bali ni kumbukumbu zile ambazo zimejikita kwenye mambo ya fursa, malengo ya muda mrefu na mfupi, aina ya maisha unayotaka kuishi miaka (mtano, kumi, ishirini au zaidi) ijayo, mambo yanayotakiwa kubadilishwa ili wewe uweze kusonga mbele, mambo unayohitaji kujifunza n.k. Ni wazi kwamba kumbukumbu za aina hii, nyingi tayari unazo kichwani, lakini hazijaweza kukusaidia pengie kwasababu, nyingine ukumbuki kama unazo kwenye kichwa chako.

Kwahiyo, mwanzo wa kuweza kupanga na kutimiza malengo makubwa katika maisha ni kuwa na kumbukumbu za mawazo mazuri lakini yaliyoandikwa kwenye karatasi, kwani huu ndiyo msingi mkubwa na mzizi mkuu wa mafanikio. Watu wengi waliofanikiwa wanasema kumbukumbu ambazo  “zimeandikwa kwenye karatasi” ndizo za uhakika na ambazo unaweza kuzitegemea  kukuongoza kwenye safari yako ya kuelekea maisha unayoyataka. Ili kuweza kupata na kutunza kumbukumbu, huitaji kuwa na kitu kingine zaidi ya “nidhamu” ya kufanya vitu rahisi na ambavyo ni vya kawaida kila siku.

Wajasiriamali waliofanikiwa wanakwambia kwamba, kama ukipata au kusikia wazo zuri kuhusu jambo fulani lenye mashiko kwenye ndoto zako, shika kalamu na daftari na uliandike maramoja. Alafu wakati wa jioni au usiku kukiwa kumetulia, jaribu kulipitia daftari lako. Fikiria wazo ambalo lilibadilisha maisha yako, wazo lililonusuru ndoa yako, wazo lililo kutoa kwenye wakati mgumu, wazo lililokusaidia ukafanikiwa. Kazi hii endelea kuifanya mara zote bila kuacha. Kwahiyo, uwe ni mkusanyaji wa mawazo mazuri, mkusanyaji wa uzoefu kwaajili ya biashara na mahusiano yako na kwa maisha yako ya mbeleni (future).

Tunahitaji kuanzia sasa tujenge utamaduni na tabia ya kuandika kila wazo zuri tunalolipata kila siku; iwe kulifikri wenyewe, kusikiaau kuona kwa marafiki au watu wengine, iwe ni kulisoma kutoka vitabuni n.k. Ili uweze kulifanikisha hili, ni vyema ukakumbuka kuwa tabia ya kuweka na kutunza kumbukumbu za mawazo mazuri katika maadishi haitakuja ghafla kwako, isipokuwa itakuja kama utaianza kuifanya taratibu lakini ukaifanya kila siku kwa kipindi kirefu, ili uweze kuizoea. Kumbuka tulipokuwa shuleni, walimu walitufundisha kuwa na daftari kwaajili ya kuandika notisi na kabla ya kuandika tulihimizwa kuanza tarehe. Na hapo mambo yote tuliyokuwa tukifundishwa tulikuwa tukiyaandika na ndiyo maana wakati wa mitihani ulipokaribia, ilikuwa ni rahisi sana kujikumbusha kwa kupitia notisi zilizoko kwenye daftari na hatimaye kuweza kufahuru mitihani.

Tunapokuwa tumemaliza shule na kuanza maisha ya kujitegemea na kujiongoza wenyewe, tunahitaji kuwa “wanafunzi wa maisha yetu” na hapa ndipo tunatakiwa kuwa na daftari maalumu la kuandika na kuweka kumbukumbu za mawazo na mipangilio mingine ya jinsi tulivyojipanga kufanikisha ndoto zetu. Uzuri wa kuwa na daftari hili, ni kwamba, ni rahisi sana kurithisha watoto wako pamoja na vizazi vingine.


Ukweli ni kwamba, inaleta changamoto sana kuwa “mwanafunzi” wa maisha yako, maisha ya mbeleni, mwisho wako (unakotaka kufika). Kumbuka utakapo amua kuwa mwanafunzi katika shule iitwayo “maisha yako” ni tofauti na shule zingine ulizowahi kusoma. Hapa katika shule ya “maisha yako”, wewe mwanafunzi ndiye kila kitu, hakuna wa kukuamsha, wala wa kukuogoza bali wewe tu ndiye unajiongoza, unajihimiza na unajiwekea presha mwenyewe. Ni kutokana na yote haya ndiyo maana daftari la kumbukumbu za mipangilio ya maisha ya ndoto yako ni muhimu sasa kuliko siku zote. Ni muhimu tuamke, na tuweke msingi imara kwaajiri ya kufikia mafanikio makubwa.

Mpendwa msomaji, endelea kuitumia vizuri MAARIFASHOP ili kujifunza mambo mbalimbali yatakayokuwezesha kupata mafanikio. Ili kupata makala mpya kila zinapochapishwa, bonyeza neno TUMA MAKALA MAARIFASHOP kisha sajiri barua pepe yako. Na kama unapenda kupata mafunzo ya kila siku kwa njia ya whatsap bonyeza neno MAFUNZO