Monday, June 15, 2015

Pesa Nyingi Inapatikana Hapa



  • Unapoamua kuwekeza nguvu kazi yako kwenye shughuli za uzalishaji ndipo unapata bidhaa.

  •  Unapokuwa na bidhaa/huduma ndipo watu wengine sasa huamua kutoa na kutuma pesa zao kwako, ili kujipatia bidhaa/huduma husika.

 Leo hii watu wengi tunahangaika, tunanungunika na tunalalamikiana juu ya kukosekana kwa pesa. Kila mtu anamtuhumu mwenzie juu ya hali duni ya maisha. Maisha duni yametokana na kukosekana kwa mahitaji. Ili binadamu apate mahitaji, kwa sehemu kubwa anahitaji pesa na hii mara nyingi inatokana na bidhaa au huduma ambazo umezalisha mwenyewe. Uzalishaji wa bidhaa au huduma zilizonyingi unategemea zaidi matumizi ya nguvukazi, ambayo chimbuko lake ni afya bora. Mtu mwenye afya bora, kwa vyovyote vile ni mtu mwenye kuwa na nguvu yakutosha kufanya shughuli mbalimbali na hasa za kiuchumi. Nguvukazi hatupewi na mtu yeyote, bali unakuwanayo kwa kuzaliwa ilimradi, uwe na utaratibu wa kujali afya yako basi!.

Kwakuwa kila mmoja wetu anamiliki na kuitawala nguvukazi yake mwenyewe, maamuzi ya kutumia nguvukazi yako kwa mtu mwenyewe. Kuna kundi la watu wanaotumia nguvukazi yao zaidi kwenye “Uzalishaji Pesa” na kuna wengine wanaitumia zaidi kwenye shughuli ambazo siyo za uzalishaji wa pesa (Non Income Generating Activities ~ NIGA). Hapa Tanzania, bado watu wengi wanawekeza nguvukazi kubwa zaidi kwenye shughuli zisizo za uzalishaji pesa. Shughuli nyingi ambazo siyo za uzalishaji pesa, zinatumia sana pesa, hali inayopelekea watu wengi kutumia kuliko wanavyozalisha pesa. Kama nguvu-kazi yetu nyingi inawekezwa zaidi kwenye shughuli ambazo siyo za uzalishaji, basi tujue kabisa kuwa tutapata bidhaa/huduma kidogo, na hatimaye tunaishia kupata pesa kidogo.

Watu wengi tunataka na tunatamani sana “maisha bora”; maisha ambayo tutakuwa na uwezo endelevu katika kupata chochote tunachohitaji kama lilivyo kusudio la Mungu kutuweka hapa duniani. Kwakuwa, maisha bora ndiyo kusudio la watu wengi, basi inatupasa tubuni mchakato wa maisha bora badala ya hali ya sasa ambayo tumejikita kwenye shughuli za kutafuta pesa ambazo hazina mpangilio. Kwa sasa ukichunguza harakati nyingi za kutafuta pesa, unagundua kuwa kila shuguli inajitegemea kiasi kwamba kukamilika kwa shughuli moja hakuna uhusiano wowote na shughuli nyingine. Jambo hili la kufanya shughuli ambazo hazina mpangilio maalumu unaolenga kupata maisha bora, ndiyo linatufanya tukose mwelekeo na hatimaye kushindwa kuyafikia maisha ya ndoto yetu. Kwahiyo, zoezi la kutafuta pesa na hatimaye maisha bora ni lazima kulifanya kuwa la ki-mchakato zaidi kuliko ki-shughuli zaidi. Kupitia fikra, utafiti, vitabu na hitoria za watu waliofanikiwa; nimejifunza kuwa, ili uweze kuyafikia maisha ya ndoto yako (maisha bora) ni muhimu upitie mchakato maalum. Mfano ni kama huu hapa chini:

AFYA BORA     NGUVUKAZI     BIDHAA     PESA     MAHITAJI     MAISHA BORA

Ukichunguza mchakato wa kupata pesa hapo juu unaona moja kwa moja kuwa pesa siyo matokeo ya mwisho ambayo binadamu anayatafuta bali pesa ni sehemu tu ya mchakato wa maisha bora. Katika mchakato wa kupata maisha bora, pesa ipo katika nafasi ya nne kati ya vitu sita muhimu ambavyo vinahitajika kupewa kipaumbele kama unataka kufanikiwa. Mafanikio makubwa yameshindikana kufikiwa na watu wengi, kwasababu ya kutilia mkazo zaidi kitu kimoja tu! ambacho ni PESA. Michakato yetu mingi ya kutafuta pesa, haitilii mkazo vitu vingine kama “afya, nguvukazi na bidhaa”. Kwa maana nyingine tunaweza kusema kuwa hatupati pesa kwasababu mara nyingi mchakato wa kutafuta pesa na hatimaye maisha bora “tunauanzia katikati”.

Unapopanga mkakati au mchakato wa kutafuta pesa na wakati huo huo ukaacha kuzingatia na kujali afya yako, basi ujue kuwa uwezekano wa wewe kupata maisha bora ni mdogo sana. Kumbuka afya bora ndio chimbuko la nguvu ulizonazo ambazo ndio hukupatia rasilimali “nguvukazi”. Unapoamua kuwekeza nguvu kazi yako kwenye shughuli za uzalishaji ndipo unapata bidhaa au huduma ambazo hugeuka kuwa pesa. Unapokuwa na bidhaa/huduma ndipo watu wengine sasa huamua kutoa na kutuma pesa zao kwako, ili kujipatia bidhaa/huduma husika. Kwahiyo, iwapo utakuwa umezalisha bidhaa nyingi utapata pesa nyingi na ni pesa hiyohiyo ambayo na wewe utaitoa na kuituma kwa watu wengine ili kupata bidhaa/huduma na hatimaye kukidhi mahitaji yako mbalimbali. Unapofikia hatua ya endelevu wa kupata kile unachohitaji kwa muda muhafaka, ni wazi kwamba unakuwa tayari umefikia maisha bora ambayo ni ya ndoto yako na hapa ndipo unaanza kupata vitu vile ulivyokuwa ukivipenda lakini ulilazimika kuviacha kwa muda ili kuruhusu mchakato wako wa maisha bora ukamilike.

Kwahiyo, tunapojiandaa kuanza safari ya kutafuta mafanikio ni lazima tujitahidi kuanza mchakato wa kutafuta maisha bora, kwa kuanza na ujenzi wa afya bora, ili itupatie nguvukazi itakayo tuwezesha kuzalisha bidhaa za kuleta pesa nyingi kukidhi mahitaji kwa kiwango endelevu na  hatimaye kufikia maisha bora ambayo ndiyo ndoto yetu.

Mpendwa msomaji, endelea kuitumia vizuri MAARIFASHOP ili kujifunza mambo mbalimbali yatakayokuwezesha kupata mafanikio. Ili kupata makala mpya kila zinapochapishwa, bonyeza neno TUMA MAKALA MAARIFASHOP kisha sajiri barua pepe yako. Na kama unapenda kupata mafunzo ya kila siku kwa njia ya whatsap bonyeza neno MAFUNZO

No comments: