Friday, April 27, 2018

Pesa na Hifadhi ya Nishati Mwilini Vinahusiana Namna Hii


Pesa yoyote halali inapatikana kwa kufanya kazi halali. Kufanya kazi kwa juhudi na maarifa kutategemea sana uwepo wa nishati au nguvu mwilini. Nishati mwilini ni kitu cha kwanza na cha msingi katika kuleta ubora wa maisha yetu. Nishati au nguvu mwilini inapatikana kutokana na vyakula tunavyokula. Pia, tufahamu kuwa nishati ipatikanayo mwilini utumika katika kufanya shughuli za ndani ya mwili na shughuli za nje ya mwili kama zile za uzalishaji mali. Tatizo lililopo kwasasa ni...
watu wengi kushindwa kutambua kuwa, hifadhi ya nishati iliyopo mwilini haitumiki katika kufikiri na kutenda shughuli za uzalishaji mali, badala yake; inatumika zaidi katika kufanya shughuli za kusaga chakula na kukabiliana na mrudikano wa sumu, ambazo zinazotokana na vyakula tunavyokula pamoja na mpangilio mbovu wa chakula.


Nishati ya kutosha mwilini inachangia kwa kiasi kikubwa sana kuchochea fikra, dhamira, shauku na utashi wa kufanya vitu vikubwa vinavyoweza kukuletea mafanikio ya kweli, hasa uhuru wa kipato na uhuru wa kuchagua kile ukipendacho maishani. Ukweli ni kwamba, “kitendo cha kukosekana kwa nishati ya kutosha mwilini ni sawa na gari lisilokuwa na mafuta”. Ili kuwa na kiwango cha juu cha nishati mwilini ni muhimu kwa wapenda mafanikio wote tukaanza utaratibu wa kula chakula kwa kufuata mzunguko (mpangilio) huu wa chakula na wa asili ndani ya miili yetu.

Tunapozungumzia mzunguko wa chakula wa asili, tunamaanisha kuanzia pale unapokula chakula hadi pale unapotoa nje zile takamwili zote au uchafu wote uliobaki baada ya ile sehemu nzuri ya ulichokula kufyonzwa tayari kwa matumizi ya kujenga na kulinda mwili wako.

Kwa ufupi mzunguko wako wa asili umegawanyika mara tatu ndani ya mzunguko wa masaa 24 (siku moja), kama ifuatavyo:

1. Mzunguko wa kukaribisha chakula: Mzunguko huu ni kuanzia saa sita mchana hadi saa mbili usiku (chakula kama matunda uliwa na kusagwa)

2. Mzunguko wa kufyonza chakula: Mzunguko huu ni kuanzia saa mbili usiku hadi saa kumi usiku/alfajiri (hapa chakula uanza kutumika mwilini)

3. Mzunguko wa kuondoa chakula: Mzunguko huu ni kuanzia saa kumi usiku hadi saa sita mchana (hapa mabaki na uchafu uliotokana na kile ulichokula uanza kutolewa nje). Ukitambua mzunguko huu wa asili na ukaweza kula kwa kuruhusu kila mzunguko kufanya kazi ipasavyo, utaweza kuruhusu hifadhi kubwa ya nishati mwilini mwako na kuona afya ya mwili uliosisimka na kuchangamka kuliko ulivyowahi kuona. Ufunguo hapa ni kuhakikisha kuwa sumu zinakuwa zimetoka nje na mwili wako kubakia safi ndani.

Ili kuruhusu kila mzunguko wa asili kufanya kazi sawasawa, unaweza kuzingatia yafuatayo:

1. Kula vyakula vyenye maji mengi
Asilimia 70% ya sayari ya dunia ni maji kama ulivyo mwili wako. Ili kusafisha mifumo yote ya mwili sawasawa na kuhakikisha iko kwenye kilele cha utendaji kazi, lazima uhakikishe lishe yako inakuwa angalau ni ya vyakula vyenye kuwa na asilimia 70% ya maji (mbogamboga na matunda). Mizunguko iliyotajwa hapo juu yote hufanyakazi vizuri zaidi, ikiwa utaipatia maji kutoka kwenye mbogamboga na matunda mara kwa mara – “kanuni ile ya kunywa glass 8 kwa siku inaleta mafuriko bure mwilini pasipokuwa na ulazima”.

2. Fanyakazi kuendana na mizunguko hiyo 3 ya chakula
Ukishakuwa unakula vyakula vyenye majimaji na vyakula vinavyoishi, lazima uhakikishe kuwa ulaji wako unaendana na hiyo mizunguko mitatu iliyotajwa hapo juu—yaani; kukaribisha chakula, kufyonza chakula na kutoa chakula (taka-mwili) nje.

Kwahiyo, unaweza kupangilia ulaji wako namna hii:
Asubuhi hadi saa sita mchana: ni kipindi ambacho mwili wako hujaribu kutoa sumu na taka-mwili zingine (uchafu). Kwahiyo, unashauliwa kula matunda peke yake. Hii, itafanya zoezi lile la kusafisha mwili kuwa la ufanisi zaidi. Nyakati za asubuhi, badala ya kuhangaika upataji wa kifungua kinywa tuliozoea, anza siku yako kwa nguvu na glass ya juisi ya machungwa au apple.

Mojawapo ya uwekezaji wa maana ambao unaweza kuufanya awamu hii, nyumbani kwako ni kununua kifaa cha kutengeneza juisi (blenda). Kwasasa kuna vitabu vingi sokoni vinavyoelezea vizuri juu ya namna ya kutengeneza juisi mbalimbali. Raha na faida itokanayo na uchanganyaji wa matunda kama “apple”, “matikitimaji” n.k. inatakiwa kubadili fikra hata za wale ambao siyo waumini na washabiki wa vyakula na vinywaji vya matunda.

Mchana na kuendelea: Wakati wa chakula cha mchana (lunch), badala ya kula vyakula vilivyokaangwa (makange), kwanini usiwe na saladi (kachumbali) ya mboga za kijani kibichi, pilipili hoho, karoti, majani ya vitunguu, nyanya? Kwahiyo, mida hii ya mchana na kuendelea, unashauliwa kula mlo ambao asilimia 70% ni mbogamboga, nafaka na matunda.

Usiku kabla ya saa mbili: Wakati wa chakula cha usiku (dinner), ongeza nyama kama ni lazima, lakini hakikisha mlo unakuwa na mbogamboga na nafaka, ili kuhakikisha kunakuwepo na kiwango timilifu cha afya na nishati.

Usiku baada ya saa mbili: Unashauliwa kutokula chochote. Endapo utakula baada ya saa mbili usiku utazuia machakato wa ufyonzaji wa virutubisho kutoka kwenye vyakula ulivyokula kuazia saa sita mchana, pia utasababisha kuziba kwa mfumo (vitundu vya kunyonya chakula). Hali ya kula baada ya saa mbili usiku inanyonya sana ile hifadhi yako ya nishati. Kwa kufuata ushauli huu, pia utaweza kupata usingizi mzuri usiokuwa ule wa kushituka shituka.

Kufanya mabadiliko ya lishe kama ilivyoelezwa hapo juu siyo jambo gumu kama linavyoweza kuonekana, isipokuwa linahitaji tu maamuzi kwa kuzingatia umuhimu wake. Kwa mfano: unahitaji kufanya vitu vichache tu kama vile; kuhakikisha vyakula vya majimaji maji vinakuwepo na kila mlo unakuwa na saladi pembeni. Lakini, asubuhi, wakati mwili unaendelea na mchakato wa kutoa taka-mwili (uchafu) ni lazima utumie matunda peke yake.

Ulaji wa namna hii, siyo kama wa fasheni au anasa bali ni kwa uhalisia. Kwahiyo, ukiweza kula kiasili, na ukala vyakula vyenye majimaji, utaweza kufanya kazi zote na vile vitu vyote ambavyo kila mara ulijisikia mchovu kuvifanya.

Katika kila tukio jaribu kuchunguza faida nyingi zilizopo kwenye lishe ya mbogamboga na matunda. Utafiti uliofanyika hivi karibuni huko nchini Finland, ni kwamba asilimia 38% ya walaji wa mbogamboga na matunda walisema kwamba walikuwa wanajisikia uchovu kidogo sana, ikilinganishwa na wale wanaokula zaidi nyama. Na walijisikia kuchangamka zaidi baada ya miezi saba.

Leo hii, unapoamua kufanya mabadiliko na mageuzi katika lishe, na kama kilichoelezwa hakiohani na mfumo wako wa maisha basi niseme kwamba kuwa hauhitaji kufanya hili zoezi kupita kiasi au kuacha kula nyama kabisa, bali wewe cha kufanya ni kupunguza taratibu ulaji wako wa nyama na kujenga mapenzi na matunda mazuri na mbogamboga nzuri. Anza kutumia na kula vyakula vya kienyeji ambavyo vinakupa radha uitakayo, vyakula visivyokuwa na nyama.

Wazo lingine la kuzingatia katika kuimalisha nishati mwilini ni suala zima la nidhamu ya “kufunga” na kufanya “tahajudi”. Hili la kufunga na kutaajudi ni mambo ambayo yamekuwepo sana hasa katika jamii za mashariki (Asia na India) kwa karne nyingi. Kufunga siyo tu kwamba ukupatia faida za kiafya bali ni mbinu inayotumika kukujengea nguvu ya utashi. Kufunga ninakokusema hapa, ni rahisi kufanya. Kwa urahisi kabisa wewe jitahidi kutenga siku moja nzima kila baada ya wiki chache na hapo kula tu mbogamboga na kunywa juisi za matunda peke yake. Kwa kufanya hivyo, utakuwa unafunga kwa kutumia njia ambayo ni ya furaha na salama zaidi kwa afya yako.

Ukweli ni kwamba, katika jamii yetu, ugonjwa unaowakabili watu wengi siyo tu malaria taifodi, ukimwi, mafua n.k; BALI ni pamoja na ukosefu wa nishati ya kutosha mwilini. Ndiyo maana watu wengi kwasasa, wanaishi katika hali ya uchovu wa kudumu yaani ni uchovu usioisha na muda mwingi watu wamechoka. Kutokana na watu wengi kuwa na uchovu muda mwingi, ndiyo sababu kazi nyingi au miradi mingi inayohitaji kufikiri haifanyiki ipasavyo au haifanyiki kabisa. Kwa maneno mengine ni kwamba wengi wanapenda kufanya vitu ambavyo ni rahisi. Ni vizuri tukatambua kuwa kazi zote za kufikiri zinatumia kiasi kikubwa sana cha nishati/nguvu ya mwili. Lakini, pia tukumbuke kuwa kazi nyingi zinazohitaji matumizi makubwa ya maarifa na fikra ndizo zenye uwezo mkubwa wa kubadili maisha yako kuwa bora zaidi.

Kama wewe ni mtu ambaye uko tayari kutafuta mafanikio makubwa hasa ya kiuchumi, ni lazima kuwekeza sana katika eneo hili la lishe na utulivu wa akili (amani kichwani). Kwa kurekebisha lishe yako, huku ukiwekeza zaidi kwenye vyakula vyenye majimaji mengi. Matokeo yake ni kwamba, viwango vya nishati ya mwili wako, uwezo wa kufikiri kwa haraka na akili iliyochangamka vyote vitaboreka kwa kiwango kikubwa sana. Mwisho utajikuta ni mtu ambaye una uwezo wa kuwa na furaha ambayo uliitaka na kuitafuta siku nyingi bila mafanikio na hatimaye, utaweza kuishi maisha ambayo siku zote ulitamani kuyaishi!

Sehemu kubwa ya makala hii imetokana na maudhui ya kitabu cha “Megaliving! 3O Days to a Perfect Life”. Kama unapenda kupata nakala ya kitabu hiki bonyeza neno NITUMIE KITABU; Utaweza kutumiwa kitabu hicho mapema iwezekanavyo.

Endelea kunufahika na MAARIFASHOP mpaka utakapohisi umefanikiwa!

Kupata mafunzo kila siku kwa njia ya whasap bonyeza neno MAFUNZO


No comments: