Friday, April 10, 2015

Siri ya Kinua Uchumi wa Kaya ni Kubadili Mtazamo Wako Juu ya Pesa

PESA NI MATOKEO YA BIDHAA NA HUDUMA; NA VYOTE HIVI UTOKANA NA KAZI
 Uchumi wa kaya hautakua iwapo kila mwaka unawazia kupata pesa bila kufikiria utazalisha bidhaa au huduma gani kwenye jamii yako, hasa jamii iliyokuzunguka, uchumi wako hauwezi kukua iwapo wewe kila mwaka unakuwepo kwenye orodha ya kaya za kupata msaada wa chakula kutoka serikalini au kwa wahisani mbalimbali. Unaposikia watu wakisema kuwa uchumi wa nchi fulani ni mkubwa, mfano: Japani, Marekani, China n.k. maana yake ni kwamba watu wa nchi hizo wamechapa kazi sana na kwa kufanya hivyo, wameweza kuzalisha bidhaa nyingi mbalimbali na hivyo kuweza kuvuna (kuchuma) kwa wingi.

Bidhaa yoyote lazima itokane na kazi na bidhaa kama bidhaa ndiyo pesa yenyewe. Mantiki hii inatukumbusha kauli aliyowahi kuitoa Rais wa zamani wa Tanzania Mwalimu Julius K. Nyerere, aliposema “Pesa Siyo Msingi wa Maendeleo” kauli hii ilikuwa ya kifalsafa zaidi, na  watu wengi wakati huo, hawakuielewa kwa mtazamo wa kwamba pesa  yoyote ambayo ni halali ni matokeo ya kazi halali. Badala yake, walio wengi waliipokea kauli hii  kwa uelewa tofauti na sana sana kwa mtazamo “hasi”. Kutokana na watu wengi kuwa na mtazamo hasi juu ya kauli hii ya pesa siyo msingi wa maendeleo, basi Mwalimu Nyerere alichukuliwa na kudhaniwa kuwa miongoni mwa watu ambao hawakupenda watanzania wapate pesa.

Falsafa ya “pesa siyo msingi wa maendeleo” bado inaendelea kupingwa hadi leo hii na kupingwa kwa falsafa hii, kunazidi kudhihilisha uelewa mdogo juu ya pesa. Na hapa ndipo tulipo jikwaa na kuanguka hasa kiuchumi, kwasababu watu wengi tunawaza kupata pesa ndipo tufanye kazi. Kaya nyingi kwa sasa zimetoa kipaumbele kwa shughuli ambazo zinaleta pesa hapo hapo (fasta) na hivyo kujikuta mwaka hadi mwaka wakiwa hawana muda tena wa kufanya vitu vyenye kuleta pesa nyingi baadae na kwa muda mrefu. Mara nyingi miradi yenye kuondoa umaskini kwenye kaya, inahitaji kuvumilia na kuwa tayari kufanya kazi bila kulipwa kwa muda huo huo (malipo baadae).

Hapo zamani wakati watu walipokuwa na mfumo wa biashara wa kubadilishana vitu moja kwa moja (bartering system), uchumi wa kaya ulikuwa imara sana, kwasababu kila mmoja ilibidi afanye kazi ili kupata bidhaa. Wakati huo, kulikuwa hakuna ujanja ujanja na ilikuwa vigumu kwa mtu kumzurumu au kuishi kwa rushwa kwani utaratibu ulikuwa ni kwamba ili upate bidhaa fulani, ulitakiwa uwe na bidhaa ya kwako. Jambo hili lililazimu kila mmoja mwenye uwezo wa kufanya kazi kuwajibika ipasavyo ndio aweze kuishi. Ni bahati mbaya sana baada ya kuingia mfumo wa pesa ambayo ukaa katikati ya muuzaji na mnunuzi wa bidhaa, watu wengi tukasahau, tukaanza kuweka nguvu na fikra nyingi kwenye kutafuta hicho kitu cha katikati “pesa” bila kukumbuka kuwa kitu ambacho huwaleta pamoja watu hawa wawili yaani muuzaji na mnunuzi, huwa siyo “pesa” bali ni BIDHAA.

Mara nyingi mtu anapouza bidhaa anapewa pesa kama uthibitisho wa kukiri kupokea bidhaa hiyo. Matatizo yanaanzia pale huyo mtu anaposahau ndani ya akili yake kuwa bado ile bidhaa anayo mikononi mwake, na cha ajabu, mtu huyo anaanza kuabudu na kuthamini sana ile “pesa” kuliko hata ile bidhaa aliyokuwanayo. Mfano: kama ni mkulima hatafikiria tena kununua mbegu bora au mbolea ili kujipanga kuzalisha mazao mengi zaidi msimu unaofuata. Kitakachotokea ni kwamba mkulima huyo atachukua pesa hizo na kufanyia vitu vingine tofauti na uzalishaji wa mazao, lakini ikumbukwe kuwa hiyo pesa anayotamba nayo ilitokana na kuuza mazao na si vinginevyo. Matokeo yake mkulima huyo, msimu unaofuata  anajikuta hana pesa tena ya kuendesha kilimo chake kwa tija zaidi na hivyo kujikuta akipata mavuno kidogo sana kuliko msimu uliopita!.

Ipo mifano mingi tu ya watu kutokuwa na tabia ya kukumbuka pesa waliyonayo ilitoka wapi na hivyo kujikuta wakitenga kiasi kidogo sana kwaajiri ya kuendeleza miradi hiyo ambayo ndio hasa uwaingizia pesa nyingi. Tunahitaji kutambua kuwa pesa tuliyonayo kuna kitu kinaileta na kwa maana hiyo tuweke nguvu zetu kwenye hicho kitu badala ya pesa yenyewe. Iwapo tutaanza kuiona pesa kwa mtazamo huu, tutakuwa tumepiga hatua kubwa kimaendeleo na kwakufanya hivyo tutakuwa tumejitenga na kundi kubwa la watu wenye mawazo ya wastani  wanaodhani pesa inapatikana kwa bahati! 

Pia, mtazamo wetu juu ya pesa ukibadilika, tutagudua kuwa huwezi kupata pesa kwa ujanja ujanja. Mambo yote haya yakifanyika, yatafanya uchumi wa kaya na taifa kwa ujumla kuweza kukua kwa kiwango cha kuridhisha. Ewe mtanzania, badili fikra zako juu ya pesa leo, tufanye kazi kwa bidii ili tuzalishe bidhaa na huduma mbalimbali, na kwa njia hii tutawezesha kaya zetu na taifa letu kuinuka kwa maana tutavuna (tutachuma) kwa wingi zaidi. Tukumbuke kuwa dhana nzima ya UCHUMI ni  kuchuma/kuvuna tulichokifanyia kazi” na hili ndilo dhumuni letu katika kupata maisha bora.

Mpendwa msomaji, endelea kuitumia vizuri MAARIFASHOP ili kujifunza mambo mbalimbali yatakayokuwezesha kupata mafanikio. Ili kupata makala mpya kila zinapochapishwa, bonyeza neno TUMA MAKALA MAARIFASHOP kisha sajiri barua pepe yako. Na kama unapenda kupata mafunzo ya kila siku kwa njia ya whatsap bonyeza neno MAFUNZO

No comments: