Sunday, May 24, 2015

Ajira Siyo Kazi ni Ajira na Kazi Siyo Ajira ni Kazi

Sasa hivi kuna tatizo kubwa sana la ukosefu wa ajira hasa kwa vijana. Ukosefu wa ajira ni jambo ambalo linazidi kuwawangisha  vichwa wadau wengi wa maendeleo na hasa serikali. Ni kweli serikali ina jukumu la kuhakikisha wananchi wake wanakuwa na shughuli ya kufanya ili kujiongezea kipato. Lakini, wakati jitihada za serikali zikiendelea, sisi wenyewe tunaodai kukosa kazi tunayo majukumu makubwa zaidi ya kufanya kuliko kutegemea watu wakutupatia ajira. Kwahiyo, ni vyema tushughulikie kwanza yale yote yaliyondani ya uwezo wetu ambayo nina imani yanaweza kuchagia kwa asilimia 80% katika kutupatia suruhisho la kudumu juu ya kero hii ya kukosa kazi. Hivyo basi, hatua ya kwanza kabisa ni kutafakari na kufikiri kwa kina juu ya tofauti iliyopo kati ya kazi na ajira. Maana unaweza kujikuta muda wako mwingi unautumia kutafuta ajira ukifikiri ni “Kazi”.

Kazi na ajira ni vitu viwili tofauti kabisa, na haviwezi kulinganishwa kwa kiwango chochote kile. Kazi inalipa sana na malipo yake mengine hayana kikomo, tofauti na ajira ambayo malipo yake ni kidogo na yanaweza kukoma muda wowote. Kitu cha ajabu kabisa ni kwamba watu wengi wanapendelea “ajira” kuliko “kazi” kwasababu, ulipohitimu elimu yako ulikaririshwa kuwa kazi inayotambulika rasimi ni ajira. Hii inatokana na mazoea ambayo tumeyajenga tokea tukiwa wadogo kuwa kazi yenye heshima ni ambayo umeajiriwa, ndiyo maana wale wote wanaofanya shughuli za kuajiriwa eti! ndio wanaitwa “Wafanyakazi”. Kwahiyo, wale wote ambao hawana ajira na hasa ajira rasimi, wanajiona na kujisikia kuwa hawana kazi na kutafuta njia usiku na mchana ili angalau siku moja waweze kuajiriwa. Hali hii, ya kushindwa kupata majibu sahii juu ya kazi ni ipi na ajira ni ipi. Matokeo yake kumeibuka makundi mawili ambayo ni kundi la wenye jukumu la kutoa ajira na kundi jingine ni la wenye kupata ajira. Kundi la wapata ajira ni wengi sana; Eti! Kazi yao ni kutafuta wapi ajira ilipo, na pale mtu anapotafuta ajira akakosa kwa muda huo, moja kwa moja anasema sina kazi! Hii inashangaza sana.

“Ajira” ni kufanya kazi ambayo siyo ya kwako, waweza kuwa unaipenda au huipendi. Watu wengine hawapendi kazi walizoajiriwa kuzifanya, lakini yawezekana  wanaendelea kufanya kazi hizo kwasababu wanalipwa pesa. Kutokana na hali hii, watu wengi hulazimika kutafuta kazi nyingine pale tu malipo yanapokuwa hayatoshelezi mahitaji ya muhusika. Mwenye kazi “mwajiri” anapokuwa amekuajiri kwenye kazi yake ambayo “siyo ya kwako”; wewe moja kwa moja unahesabika kuwa ni sehemu ya gharama za uendeshaji wa kazi au kampuni! Hii ni sawa na kusema kuwa waajiri wengi wanawaona wafanyakazi (waajiriwa) kama gharama za uzalishaji!. Hii haina maana kwamba waajiri hawawathamini waajiriwa wao, bali wakati wa kufanya tathimini ya maendeleo ya kazi inawabidi kufanya hivyo, ili kupanga mipango mikakati ya kuwezesha matunda ya kazi husika yapatikane kwa gharama nafuu.

 “Kazi” ni majumuisho ya majukumu mbalimbali ambayo kwa mwenye kazi unajiwajibisha mwenyewe katika kuyatimiza hayo uliyojipa mwenyewe, bila kutegemea kulipwa chochote mpaka matunda ya kazi hiyo yapatikane. Unapofanya kazi siyo lazima alipwe, kwasababu mara nyingi kazi inakuwa ni mchakato wako wa maisha na haupangiwi na mtu yeyote, wewe mwenyewe unajipangia ni nini ufanye, kwa malengo yapi na ni nani unamlenga kunufaika na matokeo (matunda) ya kazi yako. Iwapo matokeo ya kazi yako yanatoa suluhisho la matatizo au kero zilizopo kwenye jamii husika, basi ujiandae kulipwa malipo ambayo hayana kikomo, kwasababu watu watanunua matunda ya kazi yako, ili kukidhi mahitaji yao, hivyo ni rahisi wewe kuweza kutajirika kutajirika kupitia utatuzi wa kero na matatizo mbalimbali. 

 Kutokana na maana pana ya “kazi” tunaona kwamba kazi inaweza kupatikana popote lakini ajira haipatikani kila sehemu. Kazi ni nyingi sana ajira ni chache sana, hii inamanisha kwamba watu wanapenda vitu ambavyo vimeishapikwa tayari, kazi yao ni kupakua na isitoshe hata kwa kupakua tu! unalipwa na mwenye kazi. Kazi ni ya kudumu wakati ajira ina ukomo; kwenye kazi hakuna bosi, isipokuwa bosi wako ni malengo na ndoto zako lakini kwenye ajira kuna bosi ambaye anayo madaraka ya kuamua juu ya nini kifanyike na wakati mwingine kifanyike vipi na huyu ndiye anamiliki na kuongoza hatima ya mafanikio yako
na hasa ya kiuchumi. Kwenye kazi unachukua muda mrefu kuanza kulipwa tofauti na ajira ambayo, ukianza tu ajira yako unaanza kulipwa maramoja au mwisho wa mwezi huo huo. Pengine tofauti hii ya muda wa kulipwa kati ya mwenye kazi na mwenye ajira ndiyo inayowafanya watu wengi na hasa wasomi wa fani mbalimbali kupendela “ajira” kuliko “kazi”.

Kutengeneza na kufanya kazi kunahitaji kujitoa, ubunifu, kufikiri sana, kuvumilia na zaidi ya yote, kazi inahitai ujasiri na ninadhani ujasiri huu wa kufanya kazi bila kulipwa kwa wakati huo ndiyo mzizi mkuu wa neno “Ujasiriamali”. Kwenye ajira kila kitu ambacho unakifanya unadai ulipwe, kwahiyo, kama hakuna malipo hicho kitu au shughuli haiwezi kufanyika. Kwa uhalisia ni haki ya mwajiliwa kudai malipo ya kila nguvu anayowekeza kwenye ajira yake kwasababu, mwajiriwa kama mwajiriwa yeye hana umiliki wowote wala hisa juu ya matokeo au mapato yote ya  kile kilichozalishwa bali mwenye kumiliki hicho ni mwenye kazi. Waajiriwa hupewa sehemu ndogo sana ya kile chote kilichozalishwa. Makampuni mengi, kila mwisho wa mwaka huwa wanafunga mahesabu na kupima wamepata faida kiasi gani lakini siyo rahisi kwa mwenye kampuni kutoa gawio (dividend) kwa wafanyakazi wake kwasababu, wafanyakazi (waajiriwa) wote, wanahesabika kama sehemu ya gharama na siyo sehemu ya faida, na faida hii ndiyo motisha na kichocheo kikubwa cha yeye kuendelea kuwekeza na kutengeneza kazi nyingi ambazo zinaweza kutoa ajira kwa watu wengi zaidi. 

Kwakuwa kazi unajipatia mwenyewe, ni wakati muhafaka sasa wa kujipa kazi badala ya kusubili kupewa kazi (ajira). Tusisubili wale wakutuletea kazi, kwa maana hatujui wataleta lini na kwa malengo yapi. Tuzidi kukumbuka kuwa ajira haziwezi kuwa nyingi kama kazi zinazotengenezwa ni chache. Tuzidi kujipa kazi kwani chochote tutakachozalisha, watu wako tayari kununua, ilimradi kina manufaa kwao. Anza leo, kuanza kujitenga na watafuta ajira, pia jiepushe na tabia ya kulalamikia watu wengine kwa mambo ambayo ni majukumu yako. Kwahiyo, bila kujali umesomea nini, anza leo kufikiria ni kitu gani unaweza kukizalisha ambacho kina uwezo wa kutatua kero na changamoto mbalimbali katika jamii. Kwakufanya hivyo, utakuwa umepata suluhisho la kudumu juu ya kero ya muda mrefu ambayo ni ukosefu wakazi”.

Mpendwa msomaji, endelea kuitumia vizuri MAARIFASHOP ili kujifunza mambo mbalimbali yatakayokuwezesha kupata mafanikio. Ili kupata makala mpya kila zinapochapishwa, bonyeza neno TUMA MAKALA MAARIFASHOP kisha sajiri barua pepe yako. Na kama unapenda kupata mafunzo ya kila siku kwa njia ya whatsap bonyeza neno MAFUNZO

No comments: